Ivory Coast vs Norway 32 bora FIFA Kombe la Dunia

Ivory Coast watacheza hatua ya mtoano ya Kombe la Dunia kwa mara ya kwanza katika historia yao watakapokutana na Norway katika mchezo wa hatua ya 32 Bora utakaochezwa Jumanne usiku nchini Texas.

Ivory Coast wameonyesha kiwango kizuri tangu kuanza kwa mashindano haya, wakipata ushindi dhidi ya Ecuador na Curaçao. Walipoteza kwa mabao 2-1 dhidi ya Germany, waliomaliza kileleni mwa Kundi E, lakini walifanikiwa kumaliza nafasi ya pili wakiwa na pointi sita na hivyo kufuzu hatua ya mtoano.

Mshambuliaji wa Villarreal CF, Nicolas Pépé, alifunga mabao mawili katika ushindi wa 2-0 dhidi ya Curaçao kwenye mchezo wao wa mwisho wa hatua ya makundi. Ushindi huo uliwawezesha Ivory Coast kuweka rekodi nyingine ya kutoruhusu bao, huku wakizidi kuota ndoto ya kufanya vizuri katika ushiriki wao wa kihistoria kwenye Kombe la Dunia.

Kwa upande mwingine, Norway wanaingia kwenye mchezo huu baada ya kufungwa mabao 4-1 na France, waliomaliza kileleni mwa Kundi I. Hata hivyo, ushindi walioupata dhidi ya Iraq na Senegal ulitosha kuwavusha hadi hatua ya 32 Bora, ambapo sasa watapambana kutafuta nafasi ya kutinga hatua inayofuata.

Mshambuliaji wa Manchester City F.C., Erling Haaland, ambaye anashiriki Kombe la Dunia kwa mara ya kwanza, tayari amefunga mabao matatu katika mashindano haya. Nyota huyo mwenye umri wa miaka 25 alipumzishwa katika mchezo ambao Norway ilifungwa mabao 4-1 na France, na anatarajiwa kuwa silaha muhimu kwa taifa lake katika harakati za kufikia au kuvuka mafanikio yao ya mwaka 1998, walipofika hatua ya 16 Bora.

Kwa upande wa Ivory Coast, hii ni mara yao ya kwanza kabisa kufuzu hatua ya mtoano ya Kombe la Dunia, huku Norway wakirejea katika hatua hiyo kwa mara ya kwanza tangu fainali za mwaka 1998.

Ivory Coast wameonyesha uimara mkubwa wa kujilinda, wakiruhusu mabao mawili pekee katika mechi tatu za hatua ya makundi na kufanikiwa kutunza nyavu zao bila kuruhusu bao mara mbili. Safu yao ya ulinzi iliyo imara pamoja na viungo wenye nguvu kimwili vimekuwa msingi wa mafanikio yao hadi sasa.

Kombe la Dunia la mwaka 2026 ni la kwanza kushirikisha mataifa 48, hivyo hatua mpya ya 32 Bora inatarajiwa kuwa na ushindani mkubwa na matukio mengi ya kusisimua huku timu zikisaka kuandika historia mpya.

Ivory Coast ni miongoni mwa mataifa tisa ya Afrika yaliyofanikiwa kufuzu hatua ya mtoano. Kati ya mataifa 10 ya Afrika yaliyoshiriki mashindano haya, ni taifa moja pekee lililoshindwa kufuzu hatua ya 32 Bora, jambo linaloifanya fainali za mwaka 2026 kuwa ushiriki bora zaidi kuwahi kufanywa na bara la Afrika katika historia ya Kombe la Dunia.