Home Sports MABORESHO YA VIWANJA MUHIMU KWA MWENDELEZO WA BURUDANI

MABORESHO YA VIWANJA MUHIMU KWA MWENDELEZO WA BURUDANI

KILA leo ushindani unazidi kuwa imara ndani ya uwanja. Timu zinapata matokeo popote zinapocheza iwe nyumbani ama ugenini hilo ni jambo jema na linapaswa kuendelea.

Mipango makini ambayo inapangwa na timu pamoja na uongozi matokeo yake yanapatikana uwanjani. Sehemu muhimu ambayo inatoa matokeo kwa timu zote mbili zinazowania ushindi.

Bado ni mapema kwenye ligi kwa sasa ikiwa ni mzunguko wa kwanza. Timu zinaonyesha kuna kitu zinahitaji hasa kwa kupambana bila kuchoka iwe hivyo mpaka mwisho wa msimu pia.

Sio Mbeya, Lindi mpaka Kigoma burudani zinapatikana na kila kitu kinakwenda sawa baada ya dakika 90 wale waliojipanga vizuri wanapata kile kinachowastahili.

Kuwa kwenye mwendo wa kusuasua kwenye mechi za mwanzo liwe ni somo kwa wote waliokosa matokeo katika mechi zao. Ni muda wa kuendelea kufanya kazi kwa wakati ujao ili kupata kile kilichobora.

Hakuna timu ambayo inapanga kupata matokeo mabaya uwanjani. Ipo hivyo dakika 90 kila mchezaji anaingia uwanjani akifikiria kupata ushindi wa pointi tatu.

Jukumu la wachezaji ni kusaka ushindi katika mechi ambazo watacheza ili kufikia malengo yaliyowekwa na timu. Sio kazi rahisi kuibuka na ushindi muda wote kuna kupanda na kushuka hilo lipo wazi ila kuwa kwenye ushindani ni muhimu.

Kitachowapa ushindi katika kusaka matokeo ni kuwa na nidhamu nje na ndani ya uwanja. Hii ni mbinu ambayo imekuwa ikiwabeba wengi wanaotafuta mafanikio.

Mafanikio hayatokei ghafla bila kuwa na njia, hapana haipo hivyo kwenye ulimwengu wa mpira kinachobeba matokeo ni nidhamu.

Imekua inatokea kwamba timu ambayo inapewa nafasi ya kupata matokeo mazuri kwenye mechi fulani ama timu ambayo haipewi nafasi ya kupata matokeo mwisho wa siku kila mtu anakuja kutoamini kile ambacho anakiona.

Hili huwa linatokea kutokana na namna maandalizi namna yalivyokuwa. Wachezaji husika katika mchezo huo pale ambapo wanashindwa kuwa na nidhamu huwa wanapata matokeo ambayo huwa yanawashangaza.

Wale ambao walicheza kwa nidhamu wanapata kile ambacho wanastahili, hivyo ni muhimu pia kwa wachezaji kuzingatia nidhamu na kucheza kwa kufuata maelekezo ambayo wanapewa.

Mbali na suala la kutafuta matokeo pia sehemu ambayo inatafutiwa matokeo imekuwa ni ngumu kwa timu kuweza kupata kile ambacho wanastahili kutokana na ubovu wa miundombinu hasa viwanja.

Hapa Shirikisho la Soka Tanzania, (TFF) muhimu pia kulitazama hili kwa ukaribu kwa kuwa kuna baadhi ya sehemu ya kuchezea haziruhusu kabisa mpira kuchezeka kwa kiwango kizuri na kuwapa fursa wachezaji kuonyesha kile ambacho wanacho.

Ipo wazi kwamba kuna tatizo la viwanja vizuri vya kuchezea kwani vinahesabika lakini hata hivi ambavyo vipo vikifanyiwa maboresho huwa vinakuwa vizuri na matokeo yakapatikana.

Ukitazama namna wachezaji wanakuwa wakicheza wakiwa Uwanja wa Azam Complex, Uwanja wa Kaitaba, Uhuru na Uwanja wa Mkapa huwa kunakuwa na ladha ya kipekee na wachezaji wanaonyesha uwezo wao bila kuogopa.

Lakini viwanja vingine vimekuwa ni tatizo kwa wachezaji kuonyesha uwezo wao kwa kuwa na hofu kubwa ya kuumia pamoja na kushindwa kupeleka mbele mpira.

Bado kuna nafasi ya kuweza kufanya maboresho katika eneo hili muhimu kwa kuwa hakuna ushindi ikiwa hakutakuwa na uwanja.

Watakaopanda kwenye ligi ni lazima kujipanga ili kufanya Muda ni sasa kufanya maboresho ili kupata matokeo mazuri ndani ya uwanja na ile burudani ambayo inapendwa na mashabiki.

Previous articleGAMONDI MASTA KUWABADILISHIA MBINU WAPINZANI
Next articleKOCHA MPYA SIMBA AANZA KAZI