JEMBE LA KAZI TAYARI KUREJEA SIMBA

BAADA ya mwishoni mwa mwaka jana taarifa kusambaa kuwa Klabu ya Simba ina mpango wa kuvunja Mkataba wake na Kiungo Mganda Taddeo Lwanga baada ya kupata majeraha uongozi umetaja siku atakayorejea kikosini.

Mashabiki wataweza kumuona kwa mara nyingine tena kiungo huyo wa kazi chafu mwishoni mwa Januari hii kwa mujibu wa Ofisa Habari, Ahmed Ally.

Ally amesema:-“Thadeo Lwanga ilikuwa tusitishe mkataba wake mwezi huu kutokana na jeraha lake kuchelewa kupona na tulikuwa tayari kutafuta mbadala wake ila daktari ametuhakikishia atakuwa amepona kufikia mwisho wa mwezi huu (January)” amesema Ahmed Ally.

Urejeo wa Lwanga ni faida kubwa kwa Simba ambayo ratiba yake ni ngumu kwa miezi miwili ya hivi karibuni, wakiwa na mfululizo wa mechi nyingi katika muda mfupi.

Hivyo urejeo wa Kiungo huyo utatoa nafasi kwa Mwalimu Pablo kuwa na machaguo mengi uwanjani, na kufanya mabadiliko ya wachezaji hivyo kuwaepusha nyota wake na uchovu.

Mashabiki wa Yanga hawana hamu naye kwa kuwa aliwatungua kwenye mchezo wa fainali ya Kombe la Shirikisho, Uwanja wa Lake Tanganyika, mwisho wa reli Kigoma.