ALIYEWATUNGUA YANGA HAYUPO LEO

KUELEKEA kwenye mchezo wa Kariakoo, Dabi ambao unatarajiwa kuchezwa Uwanja wa Mkapa leo,Desemba 11,2021 yule aliyewatungua Yanga hayupo kabisa kwenye mipango ya kocha.

Kocha Mkuu wa Simba, Pablo Franco atakuwa na kibarua cha kusaka pointi tatu muhimu mbele ya Yanga huku akiwa na wachezaji wengine kabisa na atakosa huduma ya nyota wake anayeshikilia rekodi ya kuwatungua Yanga hivi karibuni.

Ni Taddeo Lwanga, nyota wa kikosi cha Simba kiungo mkata umeme hatakuwa kwenye kikosi cha Simba kitakachowavaa Yanga, Uwanja wa Mkapa leo Desemba 11 na ikumbukwe kwamba kiungo huyo aliwatungua Yanga katika mchezo wa fainali ya Kombe la Shirikisho, mwisho wa reli Kigoma, Julai 25,2021.

Lwanga yupo nje kwa muda akitibu majeraha yake ya goti ambapo aliumia alipokuwa akitumikia timu yake hiyo kwenye mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Jwaneng Galaxy.

Kuhusu mchezo wa leo Pablo amesema kuwa utakuwa mchezo mgumu lakini anahitaji kuona vijana wake wakipata ushindi.

“Utakuwa mchezo mgumu lakini tupo tayari kwa ajili ya kuona kwamba tunapata ushindi,”.