>

YANGA IJAYO BALAA ZITO

UONGOZI wa Yanga umeweka wazi kuwa msimu ujao kikosi hicho kitakuwa ni balaa kutokana na maboresho ambayo yatafanyika kwenye kila idara.

Ipo wazi kwamba Yanga ni mabingwa wa ligi wakiwa na pointi 80 baada ya kucheza mechi 30 huku mfungaji bora akiwa ni Aziz KI mwenye mabao 21 akifuatiwa na Feisal Salum mwenye mabao 19 yupo zake Azam FC.

Ali Kamwe, Ofisa Habari wa Yanga ameweka wazi kuwa wanatambua kwamba kazi kubwa ambayo ilifanyika msimu wa 2023/24 ilikuwa kubwa na kila mchezaji alikuwa imara hivyo msimu ujao kazi itakuwa kubwa.

“Nilikuwa ninahofia namna kikosi cha Yanga kilivyokuwa kwa msimu wa 2023/24 kutokana na kila mchezaji kufanya kazi kubwa kwenye kutafuta matokeo na sasa tumefanikiwa kupata kile tulichokuwa tunahitaji ambao ni ubingwa.

“Msimu ujao tutakuwa na kikosi bora ambacho hata mwenyewe ninakiogopa, tusubiri na tuone mashabiki tuzidi kuwa pamoja na kazi itakuwa kubwa kwa wakati ujao hilo linawezekana.”

Miongoni mwa wachezaji ambao wanatajwa kuwa kwenye hesabu za kuongezewa mikataba yao ni Aziz Ki, Kibwana Shomari, Bakari Nondo.