Shirikisho la Soka la Tunisia (FTF) limemtangaza rasmi Moine Chaabani kuwa kocha mpya wa timu ya taifa kwa mkataba wa miaka minne, kufuatia kampeni mbaya ya Kombe la Dunia iliyoshuhudia timu hiyo ikipoteza mechi zote tatu za hatua ya makundi.
Katika taarifa iliyotolewa Jumanne, FTF ilithibitisha uteuzi huo uliokuwa ukiripotiwa na vyombo mbalimbali vya habari kwa siku kadhaa zilizopita.
Chaabani, mwenye umri wa miaka 45, ni mmoja wa makocha wenye mafanikio makubwa katika soka la Afrika. Akiwa na Esperance Tunis, aliiwezesha klabu hiyo kutwaa mataji mawili ya Ligi ya Mabingwa Afrika pamoja na ubingwa mara tano wa Ligi Kuu ya Tunisia.
Baada ya hapo alifundisha nchini Misri kabla ya kuhamia Morocco, ambako aliiongoza RS Berkane kutwaa ubingwa wa ligi. Klabu hiyo tayari ilikuwa imethibitisha kuwa kocha huyo angeondoka kwenda kuinoa timu ya taifa ya Tunisia.
Chaabani anakuwa kocha wa nne kuiongoza Tunisia ndani ya mwaka huu na wa nane tangu Januari 2024, jambo linaloonyesha mabadiliko ya mara kwa mara katika benchi la ufundi la timu hiyo.
Licha ya kufuzu Kombe la Dunia bila kuruhusu bao lolote, Tunisia ilishindwa kufanya vizuri katika fainali hizo. Safari ya kufuzu ilianza chini ya Jalel Kadri, ikaendelea chini ya Sami Trabelsi, huku Montasser Louhichi akisimamia mechi mbili kama kocha wa muda. Katika kipindi hicho pia Faouzi Benzarti na Kais Yaakoubi walipewa nafasi kwa muda mfupi wakati wa mechi za kufuzu Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON).
Baada ya kutolewa katika hatua ya 16 bora ya AFCON mwezi Januari, Trabelsi aliondolewa na nafasi yake kuchukuliwa na Sabri Lamouchi. Hata hivyo, baada ya Tunisia kufungwa mabao 5-1 na Sweden katika mchezo wa kwanza wa Kombe la Dunia, Lamouchi alitimuliwa na nafasi yake kuchukuliwa na kocha Mfaransa, Herve Renard, ambaye naye alishuhudia timu ikipoteza mechi mbili zilizobaki za hatua ya makundi.
Chaabani alikuwa bado ana mkataba na RS Berkane hadi mwaka 2027, lakini klabu hiyo ilikubali kumwachia kutokana na umuhimu wa kuiongoza timu ya taifa. Katika taarifa yake, Berkane ilimsifu kocha huyo kwa weledi wake na mchango mkubwa alioutoa katika kuandika historia ya mafanikio ya klabu hiyo.