VAR Yawavunja Moyo Croatia, Ronaldo Apeleka Ureno Hatua ya 16 Bora Kombe la Dunia

Nahodha wa Ureno, Cristiano Ronaldo, ameendelea kuiweka hai ndoto yake ya kutwaa Kombe la Dunia baada ya kuiongoza timu yake kuibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Croatia katika mchezo wa hatua ya 32 bora.

Ureno walijikuta wakitangulia kufungwa kipindi cha pili kupitia kwa Ivan Perisic, lakini walirejea mchezoni baada ya Ronaldo kufunga bao la kusawazisha kwa mkwaju wa penalti. Hilo lilikuwa bao lake la kwanza kabisa katika hatua za mtoano za Kombe la Dunia.

Kocha Roberto Martinez alimtoa Ronaldo uwanjani wakati mchezo ukiwa bado na ushindani mkubwa, jambo lililoonekana kutomfurahisha mshambuliaji huyo mwenye umri wa miaka 41. Hata hivyo, akiwa benchi alishuhudia Goncalo Ramos akiifungia Ureno bao la ushindi katika dakika za nyongeza baada ya kupokea krosi maridadi kutoka kwa Rafael Leao.

Dakika za mwisho za mchezo ziligubikwa na utata baada ya Josko Gvardiol kufunga bao ambalo lingeipeleka Croatia katika muda wa ziada zaidi. Hata hivyo, mfumo wa VAR uliingilia kati na kubaini kuwa kulikuwa na kuotea (offside) katika mchakato wa bao hilo.

Waamuzi walieleza kuwa Igor Matanovic aligusa mpira uliopigwa na Perisic kabla haujamfikia Mario Pasalic, jambo lililomfanya Pasalic kuonekana ameotea licha ya mpira pia kumgonga beki wa Ureno, Renato Veiga. Baada ya mwamuzi wa VAR kupendekeza ukaguzi wa tukio hilo, mwamuzi wa kati aliamua kulifuta bao hilo.

Ushindi huo unaipeleka Ureno hatua ya 16 bora, ambako itakutana na majirani zao Spain katika mechi inayotarajiwa kuwa na ushindani mkubwa. Itakuwa ni marudio ya fainali ya UEFA Nations League ya mwaka 2025, ambapo Ureno waliibuka mabingwa.

Kwa upande wa Croatia, nahodha Luka Modric mwenye umri wa miaka 40 huenda amecheza Kombe la Dunia kwa mara ya mwisho, huku ndoto ya taifa hilo kuendelea na mashindano ikifikia tamati.