Timu ya taifa ya Brazil imefuzu rasmi hatua ya mtoano ya Kombe la Dunia 2026 baada ya kuichapa Scotland mabao 3-0 katika mchezo wa Kundi C uliochezwa Miami, huku nyota wake Vinicius Junior akiendelea kung’ara kwa kufunga mabao mawili.
Mshambuliaji huyo wa Real Madrid aliifungia Brazil bao la kwanza mapema dakika ya saba baada ya kutumia makosa ya safu ya ulinzi ya Scotland, kabla ya kuongeza lingine kwa kichwa mwishoni mwa kipindi cha kwanza.
Bao la tatu la Brazil lilifungwa na Matheus Cunha dakika ya 60, likihakikisha ushindi wa kishindo kwa mabingwa hao mara tano wa dunia.
Kwa ushindi huo, Brazil imemaliza kileleni mwa Kundi C na sasa itasafiri kwenda Houston, Texas kwa ajili ya mchezo wa hatua ya 32 bora utakaochezwa Juni 29 dhidi ya mshindi wa pili kutoka Kundi F.
Vinicius sasa amefikisha mabao manne katika mechi tatu za hatua ya makundi, akiwa amefunga katika kila mchezo wa Brazil. Amejiunga na rekodi iliyowahi kuwekwa na Ronaldo na Rivaldo mwaka 2002 kwa kufunga katika kila mechi ya makundi ya Kombe la Dunia.
Katika mbio za ufungaji bora wa mashindano hayo, Vinicius ana mabao manne, akiwa nyuma kwa bao moja dhidi ya Lionel Messi na sambamba na Erling Haaland pamoja na Kylian Mbappe.
Mchezo huo pia uliashiria kurejea kwa Neymar katika kikosi cha Brazil baada ya kukaa nje ya timu ya taifa kwa zaidi ya miaka miwili na nusu. Mfungaji huyo bora wa muda wote wa Brazil aliingia uwanjani dakika ya 76 na kushangiliwa kwa nguvu na mashabiki.
Kwa upande wa Scotland, matumaini yao ya kufuzu bado yapo mashakani. Wakiwa na pointi tatu na tofauti ya mabao ya -3, sasa wanasubiri matokeo ya makundi mengine ili kujua kama wataingia miongoni mwa timu bora zilizomaliza nafasi ya tatu.