GEORGE WEAH, OKOCHA WASHIRIKI MASHINDANO YA DUNIA YA VILABU VYA WACHEZAJI WASTAAFU

 WACHEZAJI mbalimbali nyota wa zamani wakiongozwa na Ronadihno Gaucho na Rais wa zamani wa Liberia, George Weah watashiriki katika mashindano ya vilabu ya Dunia Veterans Club World Championship (VCWC) yaliyopangwa kufanyika mjini, Kigali, Rwanda.

Mbali ya wachezaji hao maarufu, pia wachezaji nyota mwingine duniani, Jay Jay Okocha na Andy Cole watashiriki katika mashindano hayo kwa mujibu wa Afisa Mkuu wa Biashara wa betPawa, Ntoudi Mouyelo. Mashindano hayo yamepangwa kuanzia Septemba 1 mpaka 10.

Pia katika orodha hiyo ni Patrick Mboma, Oliver Kahn, David Trezeguet, Bacary Sagna, Louis Saha, Andy Cole, Djibril Cisse. Mashindano hayo yatashirikisha wachezaji wa zamani 150 ambapo mbali ya kuonyesha vipaji vyao uwanjani, pia watashiriki kwenye mijadala mbalimbali ikiwa pamoja na ya kiuchumi, amani, elimu, afya, biashara, na utalii.

Mouyelo amesema kuwa betPawa imeamua kudhamini mashindano hayo kutokana na kutambua umuhimu wa michezo na sekta nyingine ambazo malengo yake ni ustawi wa jamii.

“Mbali ya kwenda kushiriki Kigali, baadhi ya wachezaji hao watatembelea Tanzania na Uganda na kuendesha kliniki za michezo. Kile tunachotaka ni kusikika zaidi kwa sauti za wachezaji hawa maarufu kote barani.

Amesema kuwa kudhamini tukio hili ni njia ya kurudisha kwa jamii inayoiamini chapa yao ya betPawa na pia ni njia ya kuwaunga mkono wachezaji hao katika dhamira yao ya kuunda umoja wa wachezaji maarufu wapya kote barani.

“Kwa hivyo, tunasubiri kuona kipaji cha wachezaji kama Ronaldinho, George Weah, Jay-Jay Okocha, na wachezaji wengine wote katika tukio hili la kihistoria hapa Afrika.”

Amesema betPawa ambapo ni kampuni ya michezo ya kubashiri inayomilikiwa na kampuni ya Mchezo Limited yenye makao mjini Kigali, itashiriki kikamilifu katika tukio hilo.

Kwa upande wake, Mwanzilishi wa VCWC Fred Siewe alisema wanatarajia kuwa na wachezaji 160 kutoka nchi mbalimbali duniani.

“Wachezaji hao maarufu wote wameamua kuwa sehemu ya jukwaa hili kwa sababu mahitaji yalikuwepo.” amesema.

Siewe aliwataka mashabiki wa soka kujitokeza kwa wingi kwa ajili ya mashindano hayo na katika shughuli nyingine za kijamii na ushiriki waokatika kliniki za michezo.