AZAM FC: TUPO KAMILI GADO

UONGOZI wa Azam FC umeweka wazi kuwa upo kamili gado utapambana kufanya vizuri kitaifa na kimataifa msimu wa 2024/25 ndani ya uwanja kwa kufanya maandalizi mazuri.

Timu hiyo inanolewa na Kocha Mkuu, Yusuph Dabo imemaliza ligi ikiwa nafasi ya pili na pointi 69 sawa na Simba iliyo nafasi ya tatu baada ya ushindani mkubwa kwa wababe hao wawili wakitofautiana kwenye mabao ya kufunga na kufungwa.

Azam FC itashiriki Ligi ya Mabingwa Afrika pamoja na Yanga huku Simba na Coastal Union hizi zitashiriki Kombe la Shirikisho Afrika.

Tayari Azam FC imeanza kuwatambulisha nyota wapya ikiwa ni mzawa Adam Adam ambaye aliwahi kucheza timu ya vijana na msimu wa 2023/24 alikuwa ndani ya Mashujaa FC inayotumia Uwanja wa Lake Tanganyika Kigoma.

Ofisa Habari wa Azam FC, Hasheem Ibwe ameweka wazi kuwa mpango mkubwa wa Azam FC ni kufanya vizuri kitaifa na kimataifa kwa kuwa wapo kamili gado nje ndani.

“Tupo kamili gado kila mashindano ambayo tunashiriki tunatambua kwamba tutakuwa ndani ya Ligi ya Mabingwa Afrika hivyo maandalizi yake yatakuwa makubwa.

“Msimu uliopita tuliweka wazi kuwa tunahitaji kufanya kweli kwenye ligi ya ndani na sasa tupo Ligi ya Mabingwa Afrika nako huko pia tutafanya kweli, tupo vizuri.”