Home Sports KOCHA WA MAKIPA YANGA AFUNGUKA DIARRA KUKAA BENCHI AFCON

KOCHA WA MAKIPA YANGA AFUNGUKA DIARRA KUKAA BENCHI AFCON

KUENDELEA kusugua benchi kwa mlinda mlango namba moja wa Yanga, Djigui Diarra, akiwa na kikosi cha timu ya Taifa ya Mali inayoshiriki mashindano ya Afcon huko Cameroon, kumemuibua kocha wa makipa wa Yanga, Mbrazili, Milton Nievov ambaye ameweka wazi kuwa huenda ikaleta athari katika kiwango chake.

Diarra hajaanza katika mchezo wowote wa Mali katika hatua ya makundi kwenye Afcon, ambapo kikosi cha timu hiyo tayari kimefuzu hatua ya 16 bora na wanatarajia kuvaana na timu ya Taifa ya Equatorial Guinea keshokutwa Jumatano saa 4 usiku majira ya Afrika Mashariki.

Katika kikosi cha Yanga, Diarra ndiye mlinda mlango namba moja huku Aboutwalib Mshery akiwa ndiye namba mbili na Erick Johora ambaye ni mlinda mlango namba tatu wa kikosi hicho.

Akizungumza na Championi Jumatatu, Milton alisema: “Nilikuwa nikimtazama Diarra wakati nikiwa na Simba, naweza kusema huyu ni miongoni mwa makipa bora zaidi ndani ya Ligi Kuu ya Tanzania Bara kwa sasa na hili linathibitishwa na kuitwa kwake kwenye kikosi cha timu ya Taifa kubwa kama Mali.

“Najua hajapata nafasi ya kucheza kutokana ushindani mkubwa wa namba anaokutana nao kwenye kikosi hicho na kwa upande wetu hilo sio jambo jema, tunatamani kuona anacheza kwa sababu mara zote mchezaji anakuwa bora zaidi kadiri anavyopata nafasi ya kucheza na kukaa benchi kunaweza kuhatarisha kiwango chake japo hatuwezi kuthibitisha hilo kwa sasa mpaka atakaporejea.”

STORI: JOEL THOMAS, Dar es Salaam

Previous articleCHIKO USHINDI AMPA KIBURI NABI, USHINDANI WA NAMBA NI BALAA!
Next articleNYOTA MAN UNITED AIBUKIA SEVILLA