UWANJA WA MANUNGU CHANGAMOTO KWA SIMBA

PABLO Franco, Kocha Mkuu wa Simba amesema kuwa Uwanja wa Manungu si rafiki kwa wachezaji wake kucheza lakini wapo tayari kusaka pointi tatu.

Uwanja wa Manungu uliopo Morogoro una uwezo wa kuchukua mashabiki 25,000 na umepitishwa kuweza kutumika katika mchezo huo unaotarajiwa kuchezwa saa 10:00 jioni.

Pablo amesema:”Mchezo wetu dhidi ya Mtibwa Sugar ni muhimu kwetu kushinda na tunajua kwamba kuna changamoto katika sehemu ya kuchezea lakini hilo halitupi tabu.

“Ambacho tunakitaka ni kuona tunashinda na kwa namna yoyote tunaamini kwamba tutapa ushindi,mashabiki watarajie burudani,”.

Mchezo wa leo unatarajiwa kuwa na ushindani mkubwa kwa kuwa timu zote mbili zinasaka pointi tatu.

Mtibwa Sugar mchezo wake uliopita ilikuwa ni Januari 14 na ilitoshana nguvu kwa kufungana bao 1-1 dhidi ya Ruvu Shooting, Uwanja wa Mabatini.