POLISI TANZANIA KUKIPIGA NA YANGA ARUSHA JUMAPILI

UONGOZI wa timu ya soka ya Polisi Tanzania FC umethibitisha kupeleka mchezo wao dhidi ya Yanga SC katika Uwanja wa Sheikh Amri Abeid jijini Arusha baada ya uwanja wao wa Ushirika uliopo mjini Moshi kuwa na matumizi mengine.

 

Mchezo huo ulipangwa kupigwa Jumapili katika uwanja wa Ushirika lakini siku moja kabla ya mchezo yani Jumamosi kutakuwa na tamasha la Utamaduni Mkoa wa Kilimanjaro ambapo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan hivyo imeilazimu uongozi wa timu hiyo kuhamishia mechi hiyo Arusha.

 

Inaweza kuwa ni habari njema kwa Yanga kwani wenyewe wameweka kambi jijini hapa kujiandaa na mchezo huo na tayari juzi wametumia uwanja wa Sheikh Amri Abeid kwa mechi moja ya kirafiki dhidi ya Mbuni FC inayoshiriki ligi daraja kwanza (First league), ambapo timu hiyo iliibuka na ushindi wa mabao 2-0.