Home Sports SHIBOUB APOTEZEWA NDANI YA SIMBA

SHIBOUB APOTEZEWA NDANI YA SIMBA

BENCHI la ufundi la Simba chini ya kocha mkuu, Pablo Franco, raia wa Hispania, limeachana na mpango wa kumpa mkataba aliyekuwa kiungo wa timu hiyo kutoka nchini Sudan, Sharaf Shiboub, kufuatia kutoridhishwa na kiwango chake alichokionyesha kwenye michuano ya Kombe la Mapinduzi.

Shiboub amerejea nchini kwa ajili ya kufanya majaribio kwenye timu hiyo ambayo Alhamisi ilicheza mchezo wa fainali ya Kombe la Mapunduzi visiwani Zanzibar dhidi ya Azam FC.

Simba ilifanikiwa kushinda kwenye mchezo huo kwa ushindi wa bao 1-0 ambalo lilifungwa na Meddie Kagere kwa mkwaju wa penalti.

Ikumbukwe kiungo huyo alijiunga na Simba mwaka 2019 akitokea Al Hilal ya Sudan kabla ya kuondoka mwaka 2020 kueleka CS Constantine ambapo mwaka jana aliondoka kabla ya kurejea tena Simba kwa ajili ya majaribio hayo.

Akizungumza na Championi Ijumaa, Ofisa Habari wa Simba, Ahmed Ally, alisema kuwa mpaka sasa suala la kumpa mkataba kiungo huyo halipo kutokana na mwalimu mwenyewe kushindwa kukubaliana na kiwango chake alichokionyesha kwenye mechi za Kombe la Mapinduzi ambazo alipewa nafasi ya kucheza.

“Suala la Shiboub kuweza kupewa mkataba kiukweli hilo jambo halipo na wala hatufikirii kwa sababu mpaka sasa wachezaji ambao wanafikiriwa kuweza kupewa mkataba ni wawili ambao ni David Udoh na Moukoro Cheikh.

“Lakini suala la hao ambao nimekwambia wanaweza kupewa mkataba baada ya mchezo wa fainali kwa kuwa bado mwalimu anahitaji muda wa kuwaangalia zaidi kwa sababu katika nafasi za usajili kwa wachezaji wa kigeni imebaki moja ambayo imeachwa wazi na Duncan Nyoni ila ikiwa watasajiliwa wote wawili basi mmoja atakuwa kwa ajili ya mechi za kimataifa,” alisema Ally.

Previous articleMATOKEO YA KIDATO CHA NNE YATANGAZWA, YAPO HAPA
Next articleMAYELE ATUMA UJUMBE HUU COASTAL UNION