MTAMBO WA MABAO YANGA WAANZA KAZI

MTAMBO wa mabao ndani ya kikosi cha Yanga umeanza kazi kwa ajili ya kuivutia kasi Azam FC kwenye mchezo wa nusu fainali ya Kombe la Mapinduzi unaotarajiwa kuchezwa leo.

Januari 10,2022 Yanga ambao ni mabingwa watetezi wana kazi ya kusaka ushindi mbele ya Azam FC kwenye mchezo wa nusu fainali unaotarajiwa kuchezwa saa 10:15.

Fiston Mayele ni miongoni mwa wachezaji ambao wameanza kazi kwa ajili ya maandalizi ya mchezo wa leo pamoja Said Ntibanzokiza ambao walikosekana kwenye mechi mbili zilizopita.

Wote walikosekana kwenye mchezo dhidi ya Taifa Jang’ombe pamoja na ule wa pili dhidi ya KMKM Uwanja wa Amaan.

Razack Siwa, Kocha wa Makipa wa Yanga amesema kuwa wapo tayari kwa mchezo wa leo na kuna wachezaji ambao watakosekana katika mchezo wa leo.

“Wachezaji wapo tayari na kila mmoja yupo tayari kwa ajili ya mchezo wetu kikubwa ni mashabiki kuwa na utulivu kwa kuwa ushindani ni mkubwa,”.

Kwenye ligi, Mayele ni namba moja kwa utupiaji wa mabao akiwa ametupia mabao matano na pasi moja ya bao.