NYOTA HAWA KUTOLEWA KWA MKOPO YANGA

IKIWA kwa sasa dirisha dogo la usajili limefunguliwa nyota watatu wa Yanga wanatajwa kuwa kwenye hesabu za kutolewa kwa mkopo ili waweze kupata changamoto mpya katika timu nyingine kutokana na kukosa nafasi kikosi cha kwanza.

Nyota hao ni pamoja na Abdalah Haji, beki huyu wa kati mzawa kwenye mechi nane za Yanga amecheza mechi moja pekee na kutumia dakika mbili ilikuwa mbele ya Kagera Sugar na alitokea benchi.

Paul Godfrey naye ni beki wa pembeni katika mechi nane hajafanikiwa kuanza kikosi cha kwanza kwenye mechi hizo jambo linalomaanisha kwamba nafasi yake ni finyu.

Mabeki hawa wawili wanatajwa kuwa kwenye hesabu za Mtibwa Sugar ambayo mwendo wake umekuwa ni wa kusuasua ikiwa imecheza mechi nane imekusanya pointi tano na imefungwa mabao nane.

Mshambuliaji Yusuf Athuman akiwa amecheza mechi  tano na ametumia dakika 70 hajawa na nafasi kikosi cha kwanza jambo ambalo linafanya Biashara United kutajwa kuhitaji huduma yake.

Taarifa iliyotolewa na Yanga hivi karibuni imeeleza kuwa wapo wachezaji ambao watatolewa kwa mkopo mchakato ukikamilika hivyo mashabiki wawe watulivu.