WACHEZAJI SIMBA WAKUMBWA NA HOMA

WACHEZAJI wa Simba ambao leo wana kazi ya kusaka ushindi mbele ya Kagera Sugar kwenye mchezo wa Ligi Kuu Bara wanakabiliwa na homa pamoja na mafua.

Kwa mujibu wa Kocha Msaidizi wa Simba, mzawa Seleman Matola ameweka wazi kuwa wameweza kufika salama Kagera kwa ajili ya mchezo huo na wapo tayari lakini kuna baadhi ya wachezaji ambao wamepata changamoto kidogo.

“Nashukuru Mungu tumeweza kufika salama japokuwa tumekuwa na changamoto kidogo baadhi ya wachezaji nafikiri karibu robo tatu wamekuwa wakiugua mafua na kifua na homa za hapa na hapa sijui ni kutokana na hali ya hewa au ni nini na baadhi ya benchi la ufundi.

“Kuhusu maandalizi kila kitu kinakwenda sawa na baada ya kumaliza mchezo wetu wa Kombe la Shirikisho hapo hesabu ilikuwa ni kwenye mchezo wetu dhidi ya Kagera Sugar.

“Tunatambua kwamba utakuwa mchezo mgumu lakini tupo tayari kwa ajili ya kusaka ushindi ndani ya uwanja, mashabiki wajitokeze kuwa nasi bega kwa bega,” amesema.

Simba ipo nafasi ya pili kwenye msimamo na imekusanya pointi 18 kibindoni inakutana na Kagera Sugar iliyo nafasi ya 9 na pointi 9.