SIMBA WATUA DAR, HESABU NI DHIDI YA YANGA KWA MKAPA

WAWAKILISHI wa Tanzania kwenye mashindano ya Kimataifa, Simba tayari kwa sasa wapo kwenye ardhi ya Tanzania iliyotawala amani na upendo baada ya kumaliza kazi iliyowapeleka nchini Zambia.

Simba ilikuwa na kibarua Desemba 5 nchini Zambia kwenye Uwanja wa Heroes dhidi ya Red Arrows ambapo waliweza kukamilisha dakika 90 kwa kupoteza kwa kufungwa mabao 2-1 ambapo kwa Simba nyota wa mchezo alikuwa ni Hassan Dilunga ambaye aliweza kufunga bao.

Licha ya kunyooshwa kwa kikosi hicho kinachonolewa na Pablo Franco kiliweza kutinga hatua ya makundi kwenye Kombe la Shirikisho kwa sababu mchezo wa kwanza walikuwa na mtaji wa mabao 3-0 hivyo wametinga hatua hiyo kwa jumla ya mabao 4-2.

Kwenye mchezo wa Dar nyota wa mchezo alikuwa ni Bernard Morrison ambaye alifunga mabao mawili na pasi moja ya bao ila Zambia mambo yalikuwa magumu kwake.

Usiku wa kuamkia leo Desemba 8 kikosi cha Simba kiliweza kuwasili salama Bongo kikitokea Zambia ambapo baada ya mchezo pia kiliweka kambi ya muda na kufanya maandalizi ya mchezo wao ujao dhidi ya Yanga walipokuwa Zambia.

Mchezo huo unatarajiwa kuchezwa Desemba 11, Uwanja wa Mkapa na tayari tiketi zimeanza kuuzwa.

Miongoni mwa wachezaji ambao walikuwa na kikosi cha Simba ni pamoja na Ibrahim Ajibu, Meddie Kagere, Kibu Dennis na Beno Kakolanya.