Serena Williams ameandika sura mpya katika historia yake ya tenisi baada ya kushinda mechi yake ya kwanza ya kitaaluma tangu alipoacha mchezo huo karibu miaka minne iliyopita.
Bingwa huyo wa mataji 23 ya Grand Slam alirejea uwanjani Juni 9 katika michuano ya Queen’s Club Championship jijini London, ambapo alicheza mchezo wa wawili wawili (doubles) akiwa na chipukizi wa Canada mwenye umri wa miaka 19, Victoria Mboko.
Wawili hao walifanikiwa kuwashinda Erin Routliffe na Nicole Melichar-Martinez kwa seti 7-6, 6-2 katika mechi iliyovutia mashabiki wengi.

Serena alipokelewa kwa shangwe kubwa kutoka kwa mashabiki waliohudhuria mashindano hayo, huku mume wake Alexis Ohanian pamoja na watoto wao wawili, Olympia na Adira, wakishuhudia kurejea kwake kwa mafanikio kutoka jukwaani.
Katika mechi hiyo, Serena alionyesha kiwango kizuri kwa kupiga serve iliyofikia kasi ya maili 113 kwa saa na kuonyesha uwezo wake mkubwa uliomfanya kuwa mmoja wa wachezaji bora wa tenisi kuwahi kutokea.
Licha ya ushindi huo, Serena amesema kurejea kwake hakulengi kuthibitisha chochote kwa mtu yeyote. Akizungumza kabla ya mashindano hayo, alisema tayari ameshinda mengi katika maisha yake ya michezo na kwa sasa anafurahia safari yake mpya ndani ya tenisi.
Nyota huyo mwenye umri wa miaka 44 pia amethibitisha kuwa atashiriki michuano ya Berlin Tennis Open, huku akiacha wazi uwezekano wa kurejea kucheza mechi za mtu mmoja mmoja (singles) siku zijazo.