>

SIMBA YATOSHANA NGUVU NA WAARABU KIMATAIFA

KAMPENI ya Simba kusaka tiketi ya kutinga hatua ya makundi imeanza kwa kukutana na kisiki cha mpingo ugenini mbele ya Al Ahli Tripoli ya Libya.

Baada ya dakika 90 ubao umesoma Al Ahli Tripoli 0-0 Simba hivyo dakika 90 za mchezo wakitoshana nguvu katika mchezo uliokuwa na ushindani mkubwa.

Mashabiki wa Al Ahli Tripoli walikuwa bize kuishangilia timu yao mwanzo mwisho nafasi zakufunga walikosa kutokana na uimara wa kipa Mussa Camara huku beki Che Malone akishirikiana na Shomari Kapombe, Hamza, Zimbwe na wachezaji wengine kuhakikisha ulinzi unaimarika.

Katika eneo la ushambuliaji Simba imeonyesha ubutu ikishindwa kufanya jaribio la hatari kwa mpinzani ambapo Leonel Ateba aliyeanza kikosi cha kwanza hakukomba dakika 90 nafasi yake ilichukuliwa na Valentino Mashaka.

Mashaka alionekana kukosa utulivu ndani ya uwanja ambapo shuti pekee alilopiga kuelekea langoni lilikuwa moja akiwa nje ya 18 nalo lilikwenda nje ya lango.

Edwin Balua hakuwa kwenye ubora wake kutokana na kukosa utulivu, Joshua Mutale kwenye eneo la kiungo alikuwa na mambo mengi akiishia kucheza faulo kwa wapinzani ambao walikuwa na utulivu mkubwa hivyo benchi la ufundi lina kazi kufanya maboresho kuelekea mchezo ujao.

Imeandikwa na Lunyamadzo Mlyuka, Dizo Click.