>

ATEBA AMEANZA KAZI NA ZALI, MANULA MOTO

MSHAMBULIAJI mpya wa Simba, Leonal Ateba ameanza kazi na zali la kufunga bao moja kwenye mchezo wa kimataifa wa kirafiki dhidi ya Al Hilal ya Sudan.

Ateba alikosekana kwenye mechi zilizopita kwa kuwa alikuwa hajapata vibali vya kazi kwa mujibu wa Meneja wa Idara ya Habari na Mawasiliano Simba, Ahmed Ally rasmi Agosti 31 alipata nafasi ya kuanza kikosi cha kwanza.

Mbele ya Al Hilal Ateba alipachika bao dakika ya 25 akiwa ndani ya 18 akitumia pasi ya Ladack Chasambi ambaye alitoa kwa mguu wa kulia akiwa nje ya 18, Uwanja wa KMC, Complex Mwenge.

Ukiweka mbali Ateba kuanza kikosi cha kwanza kipa Aishi Manula amerejea ndani ya Simba na kucheza mchezo wake wa kwanza chini ya Kocha Mkuu, Fadlu Davids akitumia dakika 45 za mwanzo na kipindi cha pili ni Hussen Abel aliingia.

Kwenye dakika 45 za mwanzo Manula alionyesha ubora wake kwa kuokoa hatari mbili za moto zilizotoka kwa wapinzani wao Al Hilal.

Ilikuwa dakika ya 32 na 33 ambazo zote zililenga lango alizipangua, Shomar Kapombe hatari ya dakika ya 32 kwenye harakati za kuiondoa ilibaki ndani ya 18 ikakutana na mshambuliaji wa Al Hilal dakika ya 33 aliyerudisha langoni kwa shuti kali likaokolewa na Manula.