PROFESA JANABI AZIGEUKIA USAJILI YANGA, SIMBA

MKURUGENZI Mtendaji wa Hospita ya Taifa ya Muhimbili, Profesa, Mohamed Janabi amezigeukia Yanga, Simba, Azam FC na Coastal Union na kuzishauri kuzingatia zaidi vipimo makini kwa wachezaji wapya watakaowasajili msimu wa 2023/24.

Kauli hiyo ameitoa leo wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu uwezo wa Hospital ya Muhimbili- Mloganzila, katika tukio la kuagana na mchezaji wa zamani wa Yanga, Sunday Manara ambaye alikuwa akifanyiwa matibabu kwenye hospitali hiyo baada ya upasuaji wa goti.

Janabi amezitaka klabu hizo ambazo zinaenda kuwakilisha nchi katika michuano ya kimataifa, Yanga na Azam FC wakicheza Ligi ya Mabingwa Afrika, Simba na Coastal Union wakicheza Kombe la Shirikisho ziwekeze zaidi katika suala la kupima afya za wachezaji wanaowasajili, kwa kuangalia maeneo makuu mawili ambayo ni utimamu wa afya ya magoti na moyo.

“Hizi klabu zinatumia fedha nyingi sana kusajili wachezaji hao wa kigeni, kabla ya kuwapa mkataba wanalazimika kuwapima afya zao, Mlonganzila tupo tayari kuangalia afya za wachezaji hao wanaowasajili,” amesema na kuzitaka zisidanganyike na clip za YouTube, bali zizingatie afya.