Home Sports HOROYA AC, RAJA CASABLANCA ZAMGOMBEA PABLO

HOROYA AC, RAJA CASABLANCA ZAMGOMBEA PABLO

HOROYA AC ya Guinea, imeweka ofa nzuri kumpata aliyekuwa Kocha Mkuu wa Simba, Pablo Franco raia wa Hispania ambaye alisitishiwa mkataba wake hivi karibuni.

Mara baada ya Simba kutangaza kumsitishia mkataba kocha huyo, tetesi nyingi zilizagaa za kuhitajika na baadhi ya klabu kubwa Afrika ikiwemo Amazulu FC ya Afrika Kusini.

Wakala wa kocha huyo, Edgar Mkiteno, alitihibitisha hilo kupitia moja ya kituo kikubwa cha redio nchini kwa kusema mteja wake ana ofa tatu kati ya hizo ni Horoya na Raja Casablanca ya Morocco.

Alisema kocha huyo huenda akajiunga na Horoya kutokana na ofa nzuri aliyowekea na mshahara kwa kipindi cha miaka miwili.

Aliongeza kuwa, anaishukuru Simba kwa kukaa pamoja na Pablo kwa kipindi chote huku wakimalizana vizuri.

“Pablo alikuwa akipitia changamoto nyingi sana ndani ya Simba ikiwa ni pamoja kukosa ushirikiano kutoka kwa wenzake wa benchi la ufundi, kukosa sapoti kutoka kwa viongozi wa juu, pia ugeni wa soka la Afrika.

“Nilitegemea Simba kumpa muda zaidi ili awafikishe mbali, lakini ghafla wakachukua uamuzi mgumu wa kumsitishia mkataba.

“Hadi hivi sasa nimepokea ofa tatu kutoka kwa baadhi ya klabu za Afrika ambazo zote zimeonesha nia ya kumtaka, kati ya hizo ni Horoya ambayo huenda akajiunga nayo kutokana na mshahara mkubwa aliowekewa.

“Pia ipo Raja Casablanca na Amazulu ambayo yenyewe ilikuwa ya kwanza kutangaza ofa yao,” alisema Mkiteno.

Wakati Horoya ikiweka ofa kubwa ili ajiunge na klabu hiyo, taarifa ambazo imezipata Spoti Xtra mke wa kocha huyo anashinikiza mume wake aende Afrika Kusini ilipokuwepo Amazulu.

NA WILBERT MOLANDI, SPOTI XTRA

Previous articleJUMA MGUNDA NA KASI YAKE MEI NI MOTO
Next articleMAKOCHA WAIGOMBEA SIMBA, CV ZA KUTOSHA ZATUMWA MSIMBAZI