Home Sports PABLO AGOMEA KUPANGIWA KIKOSI

PABLO AGOMEA KUPANGIWA KIKOSI

KATIKA kuelekea Kariakoo Dabi, Kocha Mkuu wa Simba, Mhispania, Franco Pablo, ameuambia uongozi wa timu hiyo kuwa hatampanga mchezaji kwa kuangalia historia pekee.

Dabi hiyo itakayowakutanisha Simba dhidi ya Yanga, inatarajiwa kupigwa Desemba 11, mwaka huu kwenye Uwanja wa Mkapa jijini Dar es Salaam.


Pablo alijiunga na timu hiyo hivi karibuni akichukua nafasi ya Mfaransa, Didier Gomes.Taarifa zimeeleza kuwa Pablo ameuambia uongozi wa timu hiyo kuwa ili mchezaji ampe nafasi ya kucheza katika kikosi chake cha kwanza, ni lazima amuangalie uwezo wake wa uwanjani.

Mara nyingi katika mechi za watani wa jadi, viongozi wamekuwa wakidaiwa kuingilia upangaji kikosi kutokana na uzoefu wao katika mechi za namna hiyo.

Lakini chanzo chetu kilisema kuwa kocha huyo amewaambia viongozi hao ili mchezaji acheze dabi hiyo na michezo mingine ya ligi ni lazima ajiunge na kambi haraka kwa ajili ya kuangalia kiwango chake kabla ya
kumpanga.


“Pablo amewashangaza viongozi wa timu baada ya kuwaambia kuwa hatampanga mchezaji yeyote kikosini kwa kuangalia historia yake bila kumuona kiwango chake, ni katika kuelekea dabi dhidi ya Yanga.

 

“Hivyo Pablo amewataka viongozi kuhakikisha Tadeo Lwanga anarejea kambini haraka kama wanataka kumuona katika dabi na michezo mingine ya ligi na Kombe la Shirikisho Afrika.

“Lwanga yupo nchini Uganda, ambapo alienda kwa ajili ya matibabu ya majeraha yake ambayo madaktari wamempa wiki nne za mapumziko kabla ya kurejea kikosini.

“Kikubwa, kocha hajawahi kuona uwezo wa Lwanga, hivyo ameutaka uongozi kuhakikisha unamleta Lwanga haraka
kwa ajili ya kuangalia kiwango chake cha uwanjani.


“Kwani tayari kocha ameridhishwa na kiwango cha kila mchezaji, hivyo alichoahidi kwa sasa ni kuwa, hataongeza mchezaji katika kikosi cha kwanza bila kujiridhisha na uwezo wake na kwamba hapendi kumchezesha mtu kwa historia yake ya mechi za nyuma.


“Kwa maana hiyo tayari ameuomba uongozi kuhakikisha unamrejesha Lwanga, ili aungane kambini na wenzake mara tu baada ya kikosi kurejea nchini kutoka Zambia kucheza dhidi ya Red Arrows,” alisema mtoa taarifa huyo.

Akizungumzia maendeleo ya afya ya kiungo huyo, Kaimu Ofisa Habari wa timu hiyo, Ally Shatry, alisema: “Kiungo huyo bado yupo nyumbani kwao Uganda na haraka atajiunga na timu hivi karibuni.”

Leo Simba ina kibarua cha kusaka ushindi mbele ya Red Arrows kwenye mchezo wa Kombe la Shirikisho ambao ni wa marudio baada ya ule wa awali kukamilika kwa Simba kushinda mabao 3-0 Uwanja wa Mkapa.

Previous articleMUONEKANO WA UKURASA WA MBELE GAZETI LA SPOTI XTRA
Next articleLIVERPOOL ETI BILA ORIGI HAKUNA MPIRA