STARS KUKWEA PIPA BAADA YA MECHI

TIMU ya Taifa ya Tanzania, Taifa Stars kesho Novemba 11 ikimaliza kazi mbele ya DR Congo, itaelekea Madagascar kwa ajili ya maandalizi ya mwisho ya mchezo utakaopigwa Novemba 14, 2021 kusaka tiketi ya kufuzu kombe la Dunia Qatar 2022, ambapo Serikali ya Jamhuri wa Muungano wa Tanzania imetoa ndege kuelekea mechi hiyo.

 

Katibu Mkuu wa Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt. Hassan Abass amesema, Serikali itatoa ndege kwa ajili ya mchezo huo ikiwa ni kuhakikisha timu inafanya vizuri nje ya uwanja na ndani ya uwanja.

“Labda tu niwaambie Serikali katika kuhakikisha tunasapoti michezo tutatoa ndege ya kwenda na kurudi kwa ajili ya mchezo huo, ndege hiyo itabeba wachezaji na benchi lote la ufundi, viongozi, wadau wa soka na waandishi wa habari kwa lengo la kwenda kuhabarisha watanzania,” amesema.

 

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa TFF, Wilfred Kidao amesema tayari wameshaanza maandalizi ya mchezo wao ujao dhidi ya Madagascar.

 

“Tayari tumeshaanza maandalizi ya mchezo wetu ujao dhidi ya Madagascar, lengo ni kuhakikisha tunapata ushindi,” amesema.

Taifa Stars inaongoza Kundi J ikiwa na alama 7 sawa na Benin huku nafasi ya tatu ikishikiliwa na DR Congo wenye alama tano na nafasi ya nne ni ya Madagascar.