WAPENI FURAHA WATANZANIA TAIFA STARS

KAZI kubwa inapaswa kufanyika leo kwa ajili ya kuiandaa kesho nzuri na inawezekana licha ya ugumu kuwa mkubwa kila wakati kutokana na timu zote kujipanga kupata ushindi hakuna namna ni muda wa kupambania malengo.

Wachezaji wa timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars jukumu lenu ni moja kusaka ushindi kwenye mechi ambazo mtashuka uwanjani kwa kuwa ili kufikia malengo kuvuka hatua ya makundi ni lazima kushinda.

Hatua ambayo wachezaji mpo kwa sasa hamna chaguo lingine litakalowaondoa hapo mlipo zaidi ya kushinda mechi mbili zilizobaki katika hatua ya makundi.

Kuanza kwa kupoteza mchezo wa kwanza wa Kombe la Mataifa Afrika, (AFCON) dhidi ya Morocco kumeongeza mlima mwingine katika mechi zinazofuata.

Inatokea na inaumiza kulingana na vile ambavyo wachezaji mlijituma zile presha za mashabiki kwamba muda wenu umegota mwisho zibebeni kwa mikono miwili na kuwapa matokeo yale wanayoyapenda.

Matokeo wanayoyapenda mashabiki yatawaongezea furaha maradufu huku mkizidi kudumu kwenye ule ubora wenu na maajabu yenu ambayo yapo kwenye miguu yenu.

Kila mmoja ana nafasi ya kufanya vizuri na kuamini kwamba kama kuna siku ya kukosa basi na ile ya kupata ipo pia jambo la msingi ni kuendelea kupambana bila kuchoka.

Wakati uliopo ni sasa kwa kuanza na Zambia kisha DR Cong hivi vyote ni vigongo kwelikweli lakini vinafungika vilevile ikiwa mtatumia nafasi ambazo mtatengeneza.