NANI KUVUNJA REKODI YA MAYELE YANGA?

    USIKU wa deni haukawii kukucha, ndivyo unavyoweza
    kusema kwani hatimaye kivumbi cha mashindano ya
    kimataifa yaani Ligi ya Mabingwa Afrika na Kombe la
    Shirikisho Afrika kimeanza kutimua vumbi rasmi Ijumaa na kinatarajiwa kuendelea wikiendi hii.

    Kwa upande wa Tanzania Bara msimu huu tunatarajiwa
    kushirikisha timu nne katika mashindano hayo, ambapo
    timu za Yanga na Simba zinatarajiwa kutuwakilisha katika
    mashindano ya Ligi ya Mabingwa Afrika, huku Azam FC
    na Singida Fountain Gate zikituwakilisha kwenye Kombe
    la Shirikisho.

    Kwa upande wa Ligi ya Mabingwa Afrika, Simba wao
    wana faida ya kuanzia hatua ya kwanza, hivyo ni watani
    zao wa jadi Yanga ambao wataanzia hatua hii ya awali
    ambapo karata yao ya kwanza itakuwa kuvaana na AS Ali
    Sabieh Djibouti Télécom (ASAS), ya Djibout ambapo
    mchezo wa mkondo wa kwanza utapigwa leo Jumapili
    kwenye Uwanja wa Azam Complex, Chamazi.

    Hapa tunakuletea dondoo muhimu za
    mchezo huu kama ifuatavyo,

    Ugenini kama nyumbani, nyumbani ni nyumbani tu

    Kama ambavyo ilikuwa msimu uliopita dhidi ya Zalan, Yanga msimu huu pia wamepata mteremko wa michezo
    yao yote miwili ya hatua ya awali kupigwa kwenye ardhi
    ya Tanzania kutokana na maombi ya Zalan ambao
    wameomba kutumia Uwanja wa Azam Complex, kama
    Uwanja wao wa nyumbani.

    Kwa wapenzi wa ngumi hii inaweza kuwakumbusha ule
    usemi wa bondia maarufu, Karim Mandonga ambaye
    aliwahi kusema yeye akipigwa kama amepiga, na akipiga
    ndo amepiga. Hivyo kwa Yanga ugenini kama nyumbani,
    na nyumbani ni nyumbani tu.

    Nani kuvunja rekodi ya Mayele?

    Msimu uliopita kwenye kikosi cha Yanga bao la kwanza kwenye mashindano ya kimataifa lilifungwa na aliyekuwa
    straika wao mkongomani, Fiston Kalala Mayele akitumia asisti matata ya Denis Nkane dakika ya 45 ya mchezo ambao ulimalizika kwa Yanga kuibuka na ushindi wa mabao 4-0 huku Mayele akifunga Hat-trick.

    Kwa sasa Mayele hayuko ndani ya kikosi cha Yanga baada ya kukamilisha uhamisho wa kujiunga na Pyramid FC ya
    Misri. Ukiachana na straika Mzambia, Kennedy Musonda

    Yanga imesajili straika mpya, Hafiz Konkon na swali kubwa ni je, nani atavunja rekodi ya Mayele? Ikumbukwe, Mayele pia msimu uliopita alimaliza akiwa mfungaji bora wa Kombe la Shirikisho Afrika akiweka kambani mabao saba na kumzidi Ranga Chivaviro.

    Rekodi zinawabeba Yanga

    Licha ya kwamba wamekuwa na rekodi mbovu ya zaidi ya
    miaka 20 kushindwa kufuzu hatua ya makundi ya Ligi ya
    Mabingwa Afrika lakini katika mizania Yanga
    wanaonekana kuwa kwenye faida kubwa ya rekodi nzuri
    za ushiriki wao kimataifa kulinganisha na wapinzani wao.

    Mafanikio makubwa ya Yanga katika mashindano ya
    kimataifa ni kuibuka washindi wa pili wa Kombe la
    Shirikisho Afrika, rekodi ambayo wamefanikiwa kuipata
    msimu uliopita ambapo waliukosa ubingwa wa
    mashindano hayo kutokana na faida ya kanuni ya bao la
    ugenini.

    Kwa upande wa ASAS ambao licha ya kwamba hakuna
    taarifa nyingi kuwahusu kwenye mtandao lakini ni inaonekana hawana rekodi yoyote ya kuweza kucheza hatua ya makundi ya mashindano ya kimataifa japo kwa nyakati kadhaa wamefanikiwa kutawala soka la ndani na
    kushinda ubingwa wa Ligi Kuu.

    Yanga wanasemaje?

    Kuelekea mchezo huo dhidi ya ASAS, Ofisa habari wa
    Yanga, Ali Kamwe: “Nadhani mchezo huu utakuwa
    mgumu zaidi kwetu kulinganisha na michezo ya Ngao ya
    Jamii kwa kuwa hatuna taarifa nyingi kuwahusu
    wapinzani wetu.

    “Tutahitaji kuwajibika zaidi kwenye mchezo huu na
    kusahau kuhusu Ngao ya Jamii  ili kutimiza malengo ya
    kufuzu hatua inayofuata.”

    Previous articleSIMBA 1-0 DODOMA JIJI, UWANJA WA UHURU WANAPATA TABU
    Next articleSIMBA YAKOMBA POINTI TATU MBELE YA WALIMA ZABABI