YANGA V US MONASTIR LEO WAKUBWA KAZINI

    LEO ndiyo leo asemaye kesho huyo ni muongo hatimaye ile siku imewadia na kazikazi kwa wakubwa inatarajiwa kufanyika Uwanja wa Mkapa.

    Ni wenyeji Yanga chini ya kocha Nasreddine Nabi raia wa Tunisia kwenye msako wa pointi tatu dhidi ya US Monastir vinara wa kundi D wakiwa na pointi 10 wote wamecheza mechi nne.

    Hapa tunakuletea namna kazi itakavyokuwa kwa wababe hawa:-

    Mtihani mkubwa

    Mastaa wa Yanga wana mtihani mkubwa kwenye mchezo wa leo katika kutimiza majukumu yao ndani ya dakika 90 kusepa na pointi tatu pamoja na kujilinda kutokana na kasi ya wapinzani wao.

    Ufungaji

    Sio Fiston Mayele peke yake ambaye alifunga mabao mechi mbili mfululizo dhidi ya Real Bamako bali hata mabeki nao wana kazi ya kusaka ushindi kwenye mchezo huo.

    Kwa watengeneza mipango Aziz KI ambaye alitoa pasi kwenye mchezo dhidi ya Real Bamako ugenini pamoja na Kennedy Musonda ambaye amekuwa akifanya kazi kubwa kwa sasa ndani ya kikosi cha Yanga.

    Mapigo huru

    Djuma Shaban ni mzuri kwenye mapigo huru na ana pasi moja kibindoni kutokana na mapigo huru huku Aziz KI naye akiwa ni mtaalamu katika kazi hizi.

    Mbali na kuwa na kazi ya mapigo huru bado wana kazi kubwa kwenye kuzuia kufanya makosa ndani ya eneo la 18 ama kutengeneza kona nyingi kwani hili ni janga kwa Yanga.

    Mashabiki na furaha

    Furaha ya mashabiki ipo kwenye ushindi na hapa ndipo ambapo wachezaji na benchi la ufundi lina kazi ya kuonyesha ule ukubwa wa Yanga kwenye anga la kimataifa.

    Moja ya kazi kubwa na ngumu kwenye mechi za kimataifa ukipoteza nyumbani unapoteza na hali ya kujiamini hasa ukitoka kuelekea ugenini.

    Fupa gumu la mwisho

    Kete ya leo Yanga ikiyeyuka wana kazi kubwa kukutana na fupa gumu la TP Mazembe yenye hasira za kutunguliwa mabao 3-1 kwenye mchezo uliochezwa Uwanja wa Mkapa.

    Dua kwa TP Mazembe ni kuona Yanga inapoteza huku wao wakishinda mchezo wao dhidi ya Real Bamako wafufue matumaini ya kutinga robo fainali jambo ambalo kwa Yanga litaongeza presha.

    Kazikazi

    Ali Kamwe, Ofisa Habari wa Yanga amesema kuwa wanatambua ni mchezo mgumu lakini wapo tayari kupata matokeo na wachezaji watafanya kazi kubwa kusaka ushindi.

    “Moja ya mchezo mgumu na wenye kushikilia hatma yetu kutinga robo fainali hapo ni kazikazi kwa wachezaji kushirikiana kusaka ushindi na mashabiki tunaomba muzidi kuwa pamoja nasi bega kwa bega,”.

    Wagumu kinomanoma

    Ben Said

    Mastaa wa Yanga wanamkumbuka kipa Ben Said ambaye alikuwa mgumu langoni alipofanikiwa kuokoa hatari dakika ya 33,35,46 na 59 zilizokuwa zinakwenda langoni mwake.

    Mchezo uliopita dhidi ya TP Mazembe pia alianza langoni na hakutunguliwa huku akionyeshwa kadi moja ya njano kwenye mchezo huo.

    Chikhaoui

    Haykeul Chikhaoui katili kwenye mapigo huru hahitaji muda mwingi kumaliza kazi kwenye mchezo ule ugenini alitoa pasi zote za mabao.

    Ni dakika ya 10 alipiga faulo ikatumiwa na Mohamed Saghroui na pigo la kona ya dakika ya 14 aliyopiga ni Boubacar Traore aliizamisha nyavuni.

    Ni chaguo la kwanza la kocha kwani alianza kikosi cha kwanza dhidi ya TP Mazembe.

    Ouattara

    Mohamed Ouattara jamaa fulani linatisha limeenda hewani halafu limepewa kazi ya ulinzi hapo huwa linabutua tu na kutibua mipango.

    Yanga walikutana na balaa lake alipoharibu mipango dakika ya 8,20,22,23,33,39,87.

    Traore

    Boubacar Traore anakumbukwa kwenye mchezo ule wa ugenini dhidi ya Yanga alifunga bao dakika ya 15 kwa pigo la kichwa na alionyeshwa kadi ya njano dakika ya 53 baada ya kuonekana akimchezea faulo kipa wa Yanga Diarra hana shughuli ndogo.

    Alifunga kwenye mchezo dhidi ya TP Mazembe bao pekee la ushindi mapema kabisa dakika ya tatu na wapinzani wao walivuja jasho bila kuambulia hata kitu ugenini

    Previous articleIHEFU WAMEZIMA NDOTO ZA AZAM FC MAZIMA
    Next articleARSENAL YATEMBEZA 4G