KIKOSI cha Simba kina kazi ya kusaka ushindi Desemba 18,2022 Uwanja wa CCM Kirumba mchezo wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Geita Gold.
Mchezo huo ni wa kwanza kwa mzunguko wa pili kwa timu hiyo inayonolewa na Kocha Mkuu Juma Mgunda.
Mapema leo Desemba 16 kikosi hicho kimewasili Mwanza kwa ajili ya maandalizi ya mwisho ya mchezo huo wa ligi.
Katika mchezo wa mzunguko wa kwanza walipokutana Uwanja wa Mkapa, Simba ilipata ushindi wa mabao 3-0 na kusepa na pointi zote tatu.
Mgunda amesema kuwa wanatambua mechi ni ngumu na kila timu inahitaji ushindi hivyo watapambana kupata ushindi.
“Wapinzani wetu wanapambana kupata matokeo nasi tupo tayari kwa ajili ya kupata ushindi ambacho tunakifanya ni kila mmoja kutimiza majukumu yake.
“Mashabiki wawe pamoja nasi kwa kuwa mashabiki ninawaita wachezaji wetu wa 12 wamekuwa wakiongeza nguvu kwenye mapambano yetu,” amesema.
Miongoni mwa wachezaji ambao wapo kwenye msafara wa Simba ni pamoja na John Bocco, Kibu Dennis,Moses Phiri,Sadio Kanoute na Henock Inonga.