PRISONS KAMILI KUIVAA BIASHARA UNITED

KIKOSI cha Tanzania Prisons, kimejiweka sawa kuelekea mchezo wao dhidi ya Biashara United utakaochezwa leo Jumanne Machi 15,2022 kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza.

Katika mchezo huo wa Ligi Kuu Bara, Biashara itakuwa nyumbani kuwakaribisha maafande hao wa Magereza wanaoburuza mkia katika msimamo wa ligi hiyo.

Prisons na Biashara zote zipo katika hatari ya kushuka daraja, hivyo kila timu itahitaji pointi tatu muhimu ili kujiweka eneo salama.

Prisons ipo nafasi ya mwisho kwenye msimamo ikiwa na pointi 13 huku Biashara ikiwa nafasi ya 13 kwa alama 16. Ofisa Habari wa Prisons, Jackson Luka Mwafulango, amesema kikosi chao kipo tayari kuweza kufanya vizuri kwenye mchezo huo.

“Tunacheza na Biashara, maandalizi yapo vizuri na kikosi chote kilichosafiri kipo salama na tumejipanga kuchukua alama tatu muhimu kwenye mchezo huo ili tuweze kuwa kwenye nafasi nzuri Ligi Kuu Bara,” amesema Mwafulango.