KMC V AZAM FC KUKIWASHA LEO

UWANJA wa Uhuru leo unatarajiwa kuchezwa mchezo wa kukata na shoka kati ya KMC, Wanakino Boys dhidi ya Azam FC hawa matajiri wa Dar.

Utakuwa ni mchezo wa 7 kuwakutanisha kwenye mechi za Ligi Kuu Tanzania Bara ambapo rekodi zinaonyesha kwamba Azam FC wamekuwa wababe mbele ya KMC.

Azam FC ni mara tatu imeshinda huku KMC ikishinda mara moja na sare zikipatikana mara mbili na jumla yalifungwa mabao 13 ambapo Azam FC mtaji wao ni mabao 8 na KMC ni mabao matano.

Kwa mujibu wa Habib Kondo, Kocha Msaidizi wa KMC aliliambia Spoti Xtra kutokuwa na matokeo mazuri kwenye mechi zao zilizopita maandalizi yaliyofanyika yanawapa imani ya kupata matokeo mazuri.

“Kweli hatujaanza vizuri kwenye michezo yetu ila tupo kwenye ubora wete hasa kwa maandalizi ambayo tumeyafanya tunaamini kwamba yataleta matokeo chanya,” .

Kwa upande wa Vivier Bahati, Kocha Msaidizi wa Azam FC alisema kuwa kila mchezo kwao ni muhimu wanahitaji pointi tatu.

Azam FC itakosa huduma ya mtupiaji wao Prince Dube ambaye bado hajawa fiti kutokana na kusumbuliwa na majeraha pamoja na Ayoub Lyanga ambaye huyu alipelekwa Afrika Kusini kufanyiwa upasuaji na maendeleo yake kwa sasa ni mazuri.