PABLO:TUNAKWENDA KUSAKA POINTI TATU ZA RUVU SHOOTING

PABLO Franco, Kocha Mkuu wa Simba amesema kuwa wanakwenda Mwanza wakiwa wamejiandaa kushinda pointi tatu kwenye mchezo wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Ruvu Shooting unaotarajiwa kuchezwa Uwanja wa CCM Kirumba.

Leo kikosi cha Simba kimekwea pipa na kuibuka Mwanza kwa ajili ya maandalizi ya mwisho ya mchezo huo ambao unatarajiwa kuwa na ushindani mkubwa ndani ya dakika 90.

Itakuwa ni Novemba 19 ambapo mashabiki wanashauku ya kuona mbinu za Pablo kwa mara ya kwanza baada ya kuchukua mikoba ya Didier Gomes.

Pablo amesema:”Tunaamini kwamba mchezo wetu utakuwa mkubwa na hesabu ni kwenye kupata pointi tatu muhimu hivyo tupo tayari.

“Kitu pekee ambacho tunajua ni kwamba mchezo utakuwa mgumu na ushindani mkubwa, hakuna tatizo kwetu kutokana na namna ambavyo tumejiandaa hivyo tunakwenda kuona tunapata ushindi.

“Jambo pekee ambalo tunahitaji kuona ni matokeo mazuri hivyo mashabiki wawe pamoja nasi kwa kuwa jambo tunalohtaji ni matokeo,” amesema.

Simba ipo nafasi ya pili kwenye msimamo wa ligi ikiwa na pointi 11 baada ya kucheza jumla ya mechi tano.

Miongoni mwa wachezaji ambao wamesepa na kikosi ni pamoja na Meddie Kagere, Shomari Kapombe,Sadio Kanoute, Mzamiru Yassin.