KOCHA MPYA SIMBA ISHU YAKE IMEFIKIA HAPA

WAKATI Ligi Kuu Bara ikiwa imesimama kwa takribani wiki mbili, Bodi ya Wakurugenzi ya Simba, imepanga kutumia muda huo kushusha kocha mpya wa kuinoa timu hiyo ambayo pia inajiandaa na mchezo wa Kombe la
Shirikisho Afrika dhidi ya Red 
Arrows ya Zambia.

 

Novemba 28, mwaka huu, Simba itavaana na Red Arrows kwenye Uwanja wa Mkapa, Dar, ukiwa mchezo wa kwanza wa mtoano kusaka nafasi ya kwenda makundi ya michuano
hiyo, kabla ya kurudiana 
Desemba 5, nchini Zambia.

Akizungumza na Spoti Xtra, Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati ya timu hiyo, Asha Baraka, alisema kuwa bodi imepanga kumleta kocha huyo kabla ya mchezo huo wa kimataifa.


Kiongozi huyo alisema kuwa, 
kocha huyo huenda akakaa katika benchi kwenye mchezo huo ambao timu hiyo watahitaji ushindi.


Aliongeza kuwa wajumbe wa 
bodi wanatarajiwa kukutana kufanya kikao baada ya mchezo wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Namungo FC.


“Ngumu kumleta kocha mpya 
bila ya maamuzi ya pamoja ya wajumbe kukubaliana kwa pamoja baada ya kupitia CV za makocha kumi waliopitishwa katika mchujo wa awali.


“Mchujo wa mwisho 
umepangwa kufanywa haraka mara baada ya mchezo wa ligi dhidi ya Namungo tutakaocheza Uwanja wa Mkapa.


“Baada ya mchujo huo 
kufanyika haraka kocha mpya atatangazwa sambamba na kuanza kazi katika kipindi hichi
ambacho ligi imesimama,” 
alisema Baraka.

Jina la Kocha Mkuu wa Horoya AC ya Guinea, Lamine N’diaye, ndiyo linalotajwa kumrithi aliyekuwa kocha wa
timu hiyo, Mfaransa, Didier 
Gomes.