KIBWANA,SAIDO BADO HAWAJAPEWA MIKATABA

WAKATI wachezaji Kibwana Shomari na Saido Ntibazonkiza wakiwa wanafanya vyema ndani ya Yanga, habari mbaya zaidi kwa upande mwingine ni kuwa wachezaji hao bado hawajapewa mikataba mipya huku ile ya awali ikiwa inatamatika hivi karibuni.

Saido na Kibwana, wote wamekuwa katika sehemu ya kikosi cha kwanza cha timu hiyo cha kocha mkuu Mtunisia, Nasreddine Nabi, ambapo Kibwana amekuwa akitumika kama beki wa kushoto na Saido kama winga wa kushoto au kiungo mshambuliaji.

Chanzo cha ndani kutoka Yanga kimeliambia Championi Jumatatu, juu ya hofu ya Simba kufanya mazugumzo na wachezaji hao kulingana na mikataba yao kuwa katika muda wa kufanya mazungumzo na timu yoyote ambayo itawahitaji, jambo ambalo litakuwa ni pigo kwa Yanga kama watawakosa wachezaji hao.

“Kibwana na Saido wote mikataba yao ipo ukingoni na hofu kubwa zaidi ni kuingia katika mazungumzo na viongozi wa Simba ambao mara kwa mara wamewahi kuwahitaji, Yanga wanatakiwa kuwa makini sana na hili maana kwa sasa wanawaza sana ubingwa lakini wanaweza pia kuwakosa wachezaji hawa.

“Mfano kama Saido yeye amebakiza siku na wala sio mwezi, hivyo kufikia mwezi wa sita mkataba wake utakuwa umekwisha.

“Na inawezekana kuna michezo ya ligi akacheza akiwa hana mkataba kama bado hawatamuongezea mkataba mpya na kuhusu Kibwana yeye pia amebakiza mwezi mmoja na nusu hivyo utaona ni kwa jinsi gani wachezaji hawa walivyo kwenye hali ya hatari,” kilisema chanzo hicho.