MITETEMO YA MAYELE YATUMIKA KUITISHA SIMBA

UONGOZI wa Yanga umetumia mitetemo ya Fiston Mayele kuwatisha wapinzani wao wajao kwenye ligi ambao watakuwa ni Simba.

Yanga inaongoza ligi ina pointi 51 baada ya kucheza mechi 19 bila kupoteza huku Simba ambao ni mabingwa watetezi wakiwa na pointi 41 baada ya kucheza mechi 19.

Ofisa Habari wa Yanga, Hassan Bumbuli amesema kuwa uwepo wa mzee wa kutetema pamoja na wachezaji wengine ni salamu kwa wapinzani wao wote wajao ikiwa ni pamoja na wanaofuata,(Simba).

“Ninadhani kwamba kwa sasa burudani inaendelea, walimbeza Fiston Mayele na kusema ni mchezaji wa kawaida sasa kawafunga Azam FC inakuwa zawadi kwa Zakaria Thabit,ambaye alisema ni mchezaji wa kawaida.

“Kasi hii inaendelea hadi kwa wapinzani wetu hao wajao najua wanajua hivyo wajiandae katika hili mambo mazuri yanakuja na sisi tunaendelea na maandalizi,” amesema.

Zimebaki siku 19 kabla ya Yanga vinara wa ligi wenye pointi 51 kumenyana na Simba, Uwanja wa Mkapa.