UBINGWA YANGA MWANGA 85 ASILIMIA

BAADA ya ushindi wa mabao 2-1 ambao Yanga wameupata dhidi ya Azam FC Aprili 6, sasa kocha wa timu hiyo, Nassredine Nabi, anaamini wana asilimia 85 za kutwaa ubingwa msimu huu wa 2021/22.

Lakini amewasisitiza wachezaji wake waendelee kupambana ili kuhakikisha wanakamilisha asilimia zote za ubingwa msimu huu.

Yanga katika mchezo wa mzunguko wa pili tayari wamecheza michezo 5 huku yote wakifanikiwa kushinda huku katika ligi msimu huu wakiwa hawajapoteza mchezo hata mmoja.

Akizungumza kocha Nabi alisema kuwa licha ya kubaki kwa michezo mingi lakini tayari wameona mwanga wa asilimia 85 za ubingwa msimu huu huku akisisitiza kuwaambia wachezaji wake wasibweteke ili waendelee kupambana kwa ajili ya ubingwa.

“Wachezaji wanatakiwa wasibwete licha ya kupata matokeo mazuri na ya ushindi katika michezo yetu iliyopita, kwa sasa mwanga tunauona na tunaweza kusema tupo kwenye asilimia 85 za ubingwa, hivyo kilichobaki ni kuendelea kuwa bora kila siku.

“Michezo ambayo imesalia kwa sasa yote ni michezo migumu kwa kuwa ni ile ya kuamua, kuna timu hazitahitaji kushuka daraja na nyingine zinagombania vita ya nne bora, hivyo kila mchezo ni mgumu katika mzunguko huu wa pili, tuna kila sababu ya kupambania matokeo mazuri,” alisema kocha huyo.