NAMUNGO WAWEKA WAZI KWAMBA UBINGWA NI MALI YAO

KOCHA Msaidizi wa Namungo, Jamhuri Kihwelo ‘Julio’, amesema wao ndio watakaokuwa mabingwa mwisho wa msimu hata kama watu hawawapi nafasi.

Julio amesema, kila mechi ambayo wanakwenda kuicheza kwa sasa itakuwa ni kama fainali, kwa sababu wanahitaji kupata alama tatu ambazo zitawafanya wawe mabingwa mwisho wa msimu.

Namungo wanakamata nafasi ya tatu kwenye msimamo wa ligi, wakiwa na pointi 25, ambazo ni 20 nyuma ya vinara Yanga wenye pointi 45.

Akizungumza na Championi Ijumaa Julio aliweka bayana mipango yao ya kutaka ubingwa kwa kuwa wamekuwa na mipango madhubuti ya kuona hilo lengo lao linatimia kwa kuwa uwezo wa kufanya hivyo na nia wanayo.

“Namungo tunautaka ubingwa na tutaupata msimu huu, nimekuwa nikiwaambia watu kuhusu hiki mara kwa mara. Uwezo wa kufanya hivyo tunao kwa sababu ndiyo malengo tuliyojiwekea tangu tuchukue timu hii,” alisema Julio.