Nyota wa klabu ya Real Madrid, Endrick (19), na mkewe Gabriely Miranda (23) wametangaza kuwa wanatarajia mtoto wao wa kwanza, hatua iliyovutia hisia kubwa miongoni mwa mashabiki wa soka duniani.
Tangazo hilo lilitolewa kupitia mitandao ya kijamii siku ya Ijumaa, ambapo Miranda alichapisha video na picha za kihisia akiwa pamoja na Endrick, wakisherehekea ujauzito huo.
“Now there are five of us,” aliandika Miranda, akimaanisha familia yao ikijumuisha pia mbwa wao wawili. Aliongeza pia nukuu ya Biblia kutoka Zaburi 139:13: “You knit me together in the womb.”
Ndoa ya Haraka na Mahusiano Yenye Mkataba Maalum
Endrick na Miranda wamekuwa kwenye ndoa tangu Septemba 2024, baada ya kukutana muda mfupi kabla ya kuamua kufunga ndoa. Mahusiano yao pia yamewahi kuvuta umakini baada ya kufichuliwa kuwa walikuwa na kile kilichoelezwa kama “mkataba wa mahusiano,” uliokuwa na masharti mbalimbali ya tabia na maadili ndani ya uhusiano wao.
Baadhi ya masharti hayo yaliwahi kuripotiwa kujumuisha kuepuka tabia za uraibu, kujiepusha na mabadiliko makubwa ya kitabia, na kuzingatia maadili ya heshima, upendo na uelewano.
Maisha ya Soka ya Endrick
Endrick, ambaye alijiunga na Real Madrid kwa ada kubwa kutoka klabu ya Palmeiras, alihamia kwa mkopo katika klabu ya Lyon nchini Ufaransa ili kupata nafasi zaidi ya kucheza.
Ameanza kwa kiwango kizuri Lyon, akiwemo kufunga hat-trick katika ushindi wa 5-2 dhidi ya Metz, ingawa hivi karibuni muda wake wa kucheza umepungua.
