Milio ya risasi ilisikika karibu na nyumba ya mwimbaji maarufu Rihanna iliyopo katika eneo la Beverly Hills, jimbo la California nchini United States, huku polisi wakithibitisha kuwa hakuna mtu aliyejeruhiwa katika tukio hilo.
Kwa mujibu wa taarifa za polisi, mwanamke mmoja mwenye umri wa miaka 30 alisimama nje ya nyumba hiyo baada ya kushuka kutoka kwenye gari na kufyatua risasi saba kabla ya kukimbia kutoka eneo la tukio.
Maafisa wa usalama walisema kuwa mshukiwa huyo, ambaye bado hajatajwa jina lake hadharani, alifanikiwa kukamatwa takribani kilomita 12 kutoka kwenye makazi ya mwimbaji huyo baada ya operesheni ya haraka ya polisi.
Tukio hilo limetokea muda mfupi baada ya Rihanna na mpenzi wake A$AP Rocky kupata mtoto wao wa tatu. Mnamo Septemba 9, mwimbaji huyo alijifungua mtoto wa kike, na kuongeza idadi ya watoto wao kuwa watatu.
Wanandoa hao tayari wana watoto wawili wa kiume, Riot Rose Mayers na RZA Athelston Mayers.
Rihanna, ambaye jina lake halisi ni Robyn Rihanna Fenty na anatokea Barbados, alipata umaarufu mkubwa miaka ya 2000 kupitia nyimbo zilizotikisa chati za muziki duniani kama Pon de Replay na Umbrella.
Mamlaka zinaendelea na uchunguzi ili kubaini chanzo na sababu ya tukio hilo.