Simba Yaomboleza Kifo cha Baba wa Abdulrazak Hamza

Uongozi wa Simba SC umetangaza kwa masikitiko makubwa kifo cha baba mzazi wa mchezaji wake, Abdulrazak Hamza, Marehemu Mohamed Spea Hamza, kilichotokea leo asubuhi jijini Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa taarifa ya klabu hiyo, marehemu alikuwa akisumbuliwa na maradhi kwa muda mrefu kabla ya kufariki dunia asubuhi ya leo, na kuacha pengo kubwa kwa familia, ndugu na jamaa.

Taarifa hiyo imeeleza kuwa mwili wa marehemu utasafirishwa kesho asubuhi kuelekea Kigurunyembe mkoani Morogoro, ambapo jioni utafanyika mazishi kulingana na taratibu za kifamilia na kidini.

Simba SC imeungana na mchezaji wake Abdulrazak Hamza pamoja na familia nzima katika kipindi hiki kigumu cha majonzi, ikiomba Mwenyezi Mungu ailaze roho ya marehemu mahali pema peponi na awape wafiwa subira na nguvu ya kuvumilia msiba huo mzito.