>

NAMUNGO YATHIBITISHA KURIDHIA OMBI LA KUJIUZULU LA MTENDAJI MKUU

Klabu ya Namungo Fc imethibitisha kuridhia ombi la kujiuzulu la aliyekuwa Mtendaji Mkuu wa timu hiyo, Omary Kaya kufuatia mwenendo usioridhisha wa klabu hiyo iliyopokea vipigo viwili mfululizo kwenye mechi mbili za mwanzo wa msimu huu.

Namungo FC imepoteza mechi hizo dhidi ya Tabora United na Fountain Gate na mechi zote hizo Namungo FC wamefungwa katika Uwanja wao wa nyumbani Majaliwa Stadium.

“Klabu ya Namungo Fc inamshukuru kwa mchango wake kwa kipindi chote alichokuwa ndani ya Klabu kama Mtendaji Mkuu na tunamtakia Kila la kheri katika maisha yake popote aendako” imesema taarifa ya Namungo Fc.

Kupitia ukurasa wake rasmi wa Instagram Kaya ameandika ” Mimi @ommykaya siku ya leo tarehe 30 Aug 2024 nimewasilisha kwa Uongozi barua ya kujiuzulu nafasi ya Utendaji Mkuu wa Klabu ya
NamungoFC.

“Hivyo napenda kuwashukuru Uongozi, benchi la ufundi, wachezaji na mashabiki wote wa Klabu ya Namungo katika kipindi chote nilichoitumikia klabu kwa ushirikiano wao kama familia.

“Niwatakie safari njema katika kutimiza malengo ya Klabu Inshaallah’ aliandika Kaya.