>

CHAMA AANZA MAZOEZI YANGA ONA PICHA AKIWA NA PACOME

MABINGWA watetezi wa Ligi Kuu Bara kwa msimu wa 2024/25 Yanga wametuma dongo kimtindo kwa watani zao wa jadi Simba kwa kudondosha ujumbe wenye swali la mtego: “Kwa Mkapa mtakuja kweli?

Ipo wazi kwamba msimu wa 2023/24 Simba ilipoteza nje ndani mechi zote za ligi dakika 180 walipocheza na Yanga, Uwanja wa Mkapa ule wa mzunguko wa kwanza ubao ulisoma Simba 1-5 Yanga na mzunguko wa pili Yanga 2-1 Simba.

Kwenye ujumbe huo wa Yanga waliambatanisha na picha ya kiungo mshambuliaji wao mpya Clatous Chama mchezaji wa kwanza kutambulishwa Yanga ilikuwa Julai Mosi 2024 ambapo msimu wa 2023/24 alikuwa ndani ya Simba.

Chama ameonekana mwenye furaha akiwa na Pacome kiungo wa kazi ambaye watakuwa naye kwa msimu wa 2024/25 kutimiza majukumu ndani ya Yanga inayoshiriki Ligi ya Mabingwa Afrika.

Ukiweka kando Chama kuna nyota wengine ambao wametambulishwa Yanga ikiwa ni pamoja na Aziz Andambwile, Prince Dube, Khomeiny ambaye  huyu ni kipa.

Ikumbukwe kwamba Yanga msimu wa 2023/24 walimaliza ligi wakiwa nafasi ya kwanza na pointi 80 kibindoni.