Home Entertainment OSCAR PISTORIUS KUACHIWA HURU KWA MSAMAHA LEO AFRIKA KUSINI

OSCAR PISTORIUS KUACHIWA HURU KWA MSAMAHA LEO AFRIKA KUSINI

Aliyekuwa mwanariadha wa Olimpiki mwenye ulemavu, Oscar Pistorius ataachiwa huru leo kwa msamaha na kutoka gerezani nchini Afrika Kusini baada ya kukaa jela kwa takribani miaka 11 kwa kosa la kumuua mpenzi wake Reeva Steenkamp.

Alimpiga risasi kadhaa kupitia mlango wa bafuni mwaka wa 2013 na kudai kuwa alidhani ni mwizi.

Pistorius, ambaye sasa ana umri wa miaka 37, alipatikana na hatia ya mauaji mwaka 2015 baada ya mahakama ya rufaa kubatilisha hukumu ya awali ya mauaji bila kukusudia.

Hata akiachiwa huru, bado ataishi chini ya masharti magumu mpaka kifungo chake kitakapomalizika mwaka 2029.

Kwa sheria za Afrika Kusini, wahalifu wote wana haki ya kuachiwa huru kwa msamaha mara tu watakapokuwa wametumikia nusu ya kifungo.

Pistorius aliingia gerezani Oktoba 2014, alipohukumiwa kwa mara ya kwanza.

Miguu yake ya chini ilikatwa alipokuwa chini ya umri wa mwaka mmoja.

Baadaye Pistorius alitegemea vifaa bandia na akawa mwanariadha mashuhuri duniani anayejulikana kama “blade runner.”

Alikuwa na mafanikio kwenye Michezo ya Olimpiki ya Walemavu, akishinda medali nyingi za dhahabu, na kisha akaimarisha sifa yake baada ya kushindana na wanariadha wasio na ulemavu kwenye Michezo ya Olimpiki ya London 2012.

Idara ya huduma za kurekebisha tabia nchini Afrika Kusini ilisema licha ya umaarufu wa nyota huyo wa zamani atachukuliwa kama mtu mwingine yeyote.

Hii ina maana kwamba atafungiwa nyumbani kwake kwa saa fulani za mchana na atapigwa marufuku kunywa pombe. Pia haruhusiwi kuzungumza na vyombo vya habari.

Previous articleUKURASA WA MBELE GAZETI LA CHAMPIONI IJUMAA, JANUARI 05, 2024
Next articleANAMUONDOA NYOTA YANGA KIKOSI CHA KWANZA HUYU