KWA NINI TEN HAG ANAHUKUMIWA?

    ILIKUWA  April 14, 2012, miaka 11 nyuma. Kwenye mechi kati ya Pescara dhidi ya Livorno. Mchezaji Piermario Morosin, alipatwa na mshtuko wa moyo na kuanguka uwanjani.

    Baada ya juhudi kubwa za madaktari kuokoa uhai wake, saa moja na nusu mbele, aliaga dunia. Wanasema ni jukumu la daktari kutibu, kuponya ni kazi ya maulana.

    Unajua kilichotokea baada ya kifo hicho? Watu walipoteza kazi zao, na kama haitoshi waliupoteza na uhuru wao pia.

    Hakimu Laura D’arcangelo, kwenye file lake la mashtaka, alimaliza kwa kumuweka ndani daktari wa dharula kifungo cha mwaka mmoja.

     Daktari mkuu wa Livorno, Manrilo Porcellin na daktari wa Pescara Ernesto Sabatini kwa pamoja walifungwa kifungo cha miezi 8 gerezani.

    Lilikuwa ni tukio la ajabu sana, ambalo huwa inatokea sana kwenye maisha yetu. Kuweka juhudi kwenye kitu, kisha mwisho kuambulia matokeo ya lawama.

    Kujitoa kwenye vingi, kisha mwisho kuonekana hakuna la maana ulilolifanya. Hiki ndio kitu kikubwa kinachoenda kumtokea Eric Ten Hag, kama sauti za wasiompenda zikipata sikio lenye mamlaka.

    Umeona kinachoendelea Man United? Wanapitia maisha magumu sana. Mechi zao wanashinda kwa tabu sana na mwisho kidole ananyooshewa kocha wao.

    Hakuna anayetaka kujua kuwa ni mechi ya 12 sasa, lakini tayari Man United wamepoteza zaidi ya wachezaji 8 wa kikosi cha kwanza kwa sababu ya majeruhi.

    Hakuna anayetaka kufahamu kuwa Newcastle United muda huu wanateseka kwa sababu ya majeruhi,

    Liverpool waliofanya vibaya msimu uliopita kwa sababu ya majeruhi, Arsenal baada ya kumpoteza Saliba wakapoteana msimu uliopita.

    Man City alimpoteza Rodri na akajikuta anapoteza mechi mbili, kwanini ikitokea kwa Man United, basi mbuzi wa kafara ni kocha?

    Ni kweli labda kosa lake ni kusimamia nidhamu kwa wachezaji tuwapendao. Presha kubwa anayopitia ni kutoka kwa mashabiki wa Ronaldo, De Gea, Sancho.

    Mchezaji asipompanga, vyombo vya habari vinaleta ajenda kuwa kuna bifu, wakati ni uhalisia Varane kashuka kiwango chake na kasi yake imepungua.

    Alimtaka beki wa kati, akaletewa John Evans, akamtaka De Jong wakamletea Sabtzer. Leo anajitahidi kupata matokeo pamoja na ufinyu wa kikosi chake, huzuni watu wanataka na yeye afukuzwe.

    Tan Hag ananikumbusha kisa cha wale madaktari waliohukumiwa kwa kushindwa kuponya ilihali kazi yao ni kutibu.

    Previous articleTAIFA STARS KAMILI GADO KWA KAZI
    Next articleMESSI, RONALDO, NANI MBABE WA KUAMUA MECHI UWANJANI?