WAKALI WA PASI ZA MWISHO BONGO HAWA HAPA

    KWENYE mitupio ya mabao ambao hutazamwa kwa ukaribu yule mtu wa mwisho kutokana na kazi anayofanya ndani ya uwanja katika kutupia.

    Ipo wazi kwamba mabingwa wa ligi msimu wa 2022/23 ni Yanga ambao wametwaa ubingwa huo wakiwa na pointi 74.

    Yanga ina mechi mbili mkononi za kukamilisha mzunguko wa pili.

    Haitokei bahati mbaya ngoma ikazama kambani huwa kunakuwa na muhusika mwingine nyuma ambaye anatengeneza mipango kwa ajili ya ushindi.

    Kila timu ina wataalamu wao na hapa kwenye mwendo wa data tunakuletea baadhi ambao wamekuwa wakitisha kwenye matengenezo ya pasi za mwisho namna hii:-

    Chama-14

    Clatous Chama nyota anayekipiga ndani ya kikosi cha Simba ni namba moja kwenye kutengeneza pasi za mwisho akiwa nazo 14 kibindoni.

    Rekodi zinaonyesha kuwa kwenye pasi hizo za mwisho kipindi cha kwanza alitoa jumla ya pasi saba na kipindi cha pili mbali na pasi hizo za mabao na yeye kibindoni kafunga mabao manne kati ya mabao 67 yaliyofungwa na timu hiyo.

    Ntibanzokiza

    Saido Ntibanzokiza yupo zake ndani ya Simba akiwa na pasi 12 kibindoni ndani ya ligi ambapo kwenye pasi hizo sita alitoa akiwa ndani ya kikosi cha Geita Gold na ametoa pasi sita akiwa ndani ya Simba naye kagawika nusu nusu.

    Kwenye mchezo dhidi ya Ruvu Shooting Uwanja wa Azam Complex alitoa pasi mbili za mabao na mtupiaji alikuwa ni Pape Sakho

    Lyanga

    Ukiitaja Azam FC unataja mtambo Ayoub Lyanga ambaye ni mzawa huyu katoa pasi 7 za mabao ndani ya kikosi hicho ambacho kilifunga mabao 45 baada ya kucheza mechi 28.

    Sabilo

    Mzawa mwingine mwenye namba kubwa ya kutengeneza pasi za mwisho ni Sixtus Sabilo yupo zake ndani ya Mbeya City yenye maskani yake pale Mbeya inatumia Uwanja wa Sokoine.

    Ni pasi saba kibindoni katengeneza wakati ubao wa Uwanja wa Nyankumbu ukisoma Geita Gold 0-1 Mbeya City alitoa pasi yake ya 7.

    Ni mabao 9 kafunga nyota huyu kati ya 31 ambayo yamefungwa na timu hiyo kwenye ligi baada ya kucheza mechi 28.

    Kapombe

    Shomari Kapombe beki wa Simba kahusika kwenye mabao 8 ndani ya ligi akiwa ametoa pasi sita za mabao na kufunga mabao mawili ni miongoni mwa mabeki wenye pasi nyingi.

    Mohamed

    Mohamed Hussen nahodha msaidizi wa Simba katoa pasi sita za mabao ambapo pasi yake ya sita ilikuwa Uwanja wa Azam Complex alipompa mtaalamu Clatous Chama.

    Kichuya

    Kichuya Shiza yupo zake Namungo inayotumia Uwanja wa Majaliwa kwenye mechi za nyumbani katengeneza pasi tano za mabao ndani ya kikosi hicho sawa na Mzamiru Yassin wa Simba, Desu Kaseke wa Singida Big Stars na wote ni washakji.

    Imeandikwa na Dizo Click na kutoka gazeti la Championi Jumatatu.

    Previous articleYANGA KAZI BADO HAIJAGOTA MWISHO
    Next articleNABI AFURAHIA MASHABIKI WA MARUMO