Home Sports AZAM FC WATASAJILI NAMNA HII

AZAM FC WATASAJILI NAMNA HII

KATIKA kuhakikisha wanakuwa na kikosi imara kuelekea msimu ujao wa 2022/23, uongozi wa Azam FC umejipanga kufanya maboresho makubwa kwenye kikosi chao ili wajiweke kwenye nafasi nzuri ya kutwaa ubingwa baada ya kuukosa msimu huu.

 Azam FC imekuwa na mwenendo wa kupanda na kushuka kwenye Ligi Kuu Bara huku pia kikosi hicho kikitupwa nje kwenye michuano ya Kombe la Shirikisho la Azam (ASFC) hatua ya nusu fainali.

 Mkuu wa Idara ya Habari ya Azam FC, Thabit Zakaria ‘Zaka Zakazi’ alifunguka kwamba: “Hatukuwa na msimu bora, malengo yetu yalikuwa ni kutwaa ubingwa, lakini hatujafanikiwa, hivyo tupo kwenye mikakati ya kufanya maboresho makubwa kwenye kikosi chetu.

“Tunasubiri ripoti ya mwalimu baada ya msimu kumalizika kuona ni wapi tunapaswa kufanya maboresho, ni wachezaji gani tunapaswa kuwaongeza kikosini, watakaotolewa kwa mkopo na ambao tutawaacha kwa kuzingatia maslahi ya pande zote mbili.

 “Usajili wetu utazingatia mahitaji ya benchi la ufundi kwa kiasi kikubwa na hatutasajili kwa mbwembwe kama wenzetu wanavyofanya, kikubwa mashabiki wetu wawe watulivu msimu ujao tunakuja tukiwa imara zaidi.”

Mchezo uliopita wa ligi Azam FC ilishinda mabao 2-0 dhidi ya Dodoma Jiji kete yao ya mwisho itakuwa dhidi ya Biashara United mchezo unaotarajiwa kuchezwa Uwanja wa Azam Complex.

Previous articleKOCHA WA MANULA APATA DILI AFRIKA KUSINI
Next articleSAUTI:KMC WAPANIA KUFUNGA MSIMU NA REKODI