MANULA REKODI YAKE YATIBULIWA

REKODI ya kipa namba moja wa Simba kuweza kucheza mechi nyingi bila kufungwa imetibuliwa na nyota wa Ruvu Shooting, Elias Maguli baada ya kumtungua walipokutana Uwanja wa CCM Kirumba wakati ubao uliposoma Ruvu Shooting 1-3 Simba.
Manula alikuwa ni namba moja kwa makipa ambao hawajafungwa kwenye mechi nyingi za Ligi Kuu Bara ambapo alikuwa amecheza jumla ya mechi tano ambazo ni dakika 450 bila kufungwa rekodi ambayo ilikuwa ni bora kwake.
Mshindani wake mkubwa alikuwa ni Diarra Djigui wa Yanga ambaye kwa sasa ana clean sheet nne kwenye mechi sita kwa kuwa alifungwa pia kwenye mchezo dhidi ya Namungo FC wakati ubao wa Uwanja wa Ilulu Lindi uliosoma Namungo 1-1 Yanga na bao lake la kwanza kufungwa Bongo kwenye ligi ilikuwa mbele ya Ruu Shooting ambapo ni Shaban Msala alimuachia msala.
Manula anapambana kuweza kutetea tuzo ya kipa bora kwa kuwa aliitwaa tuzo hiyo msimu wa 2020/21 baada ya kufanya vizuri na kukusanya clean sheet 18 hivyo ana kazi kubwa ya kuweza kutetea tuzo hiyo.
Tayari amecheza mechi sita na amekusanya clean sheet tano kwenye mechi alizocheza huku akiwa bado ni namba moja kwa makipa ambao wamefungwa mabao machache kwenye mechi sita ndani ya ligi.
Dakika zake 90 mbele ya Kocha Mkuu, Pablo Franco alikwama kuweza kuokoa mchomo uliopigwa ndani ya 18 na Maguli jambo ambalo limetibua rekodi yake mapema kwa kuwa chini ya Kocha Mkuu, Didier Gomes na hata mikoba ilipokuwa mikononi mwa Hitimana Thiery pamoja na Seleman Matola hakuweza kufungwa.
Kikosi cha Simba kwenye msimamo kipo nafasi ya pili kimekusanya pointi 14 huku vinara wakiwa ni Yanga wenye pointi 16 baada ya kucheza mechi sita.