YANGA KUWEKA KAMBI SHINYANGA KWA AJILI YA SIMBA

VINARA wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Yanga wenye pointi 64 wanatarajiwa kuweka kambi mkoani Shinyanga kwa ajili ya maandalizi ya mchezo wa Kombe la Shirikisho dhidi ya Simba.

Huu ni mchezo wa hatua ya nusu Fainali ya Kombe la Shirikisho ambapo mabingwa watetezi ni Simba walitwaa taji hilo walipocheza fainali na Yanga, Uwanja wa Lake Tanganyika kwa ushindi wa bao 1-0.

Jana, Mei 24 Yanga ilikuwa na kibarua cha kusaka ushindi mbele ya Biashara United na mchezo huo ulikamilika kwa sare ya kufungana bao 1-1, Uwanja wa CCM Kirumba.

Leo Mei 25 kikosi cha Yanga kimeanza safari kuelekea Shinyanga ambapo kitaweka kambi kwa ajili ya mchezo wao ujao dhidi ya Simba.

Cedrick Kaze,Kocha Msaidizi wa Yanga amesema kuwa wanatambua mchezo wao ujao utakuwa ni mgumu ila watajitahidi kusaka ushindi.

“Tunajua kwamba mchezo wetu ujao utwakuwa ni wa nusu fainali dhidi ya Simba, tunawaheshimu wapinzani wetu na tutafanya maandalizi vizuri,”.