KAZI YA SIMBA MISRI IMEKAMILIKA, ZAWADI INARUDI BONGO

UONGOZI wa Simba umeweka wazi kuwa wamekamilisha kambi yao nchini Misri kwa mafanikio wanarejea kuwapa furaha mashabiki wao.

Agosti 3 itakuwa ni kilele cha Simba Day na tayari wamefanya uzinduzi wa uzi mpya ilikuwa Julai 24 2024, kwenye hifadhi za Mikumi, Morogoro.

Simba chini ya Kocha Mkuu, Fadlu Davids ni mechi tatu za kirafiki ilicheza nchini Misri na kupata ushindi kwenye mechi zote hizo ikiwa ni mwanzo mzuri kwa kocha mpya wa Simba.

Ahmed Ally, Meneja wa Idara ya Habari na Mawasiliano Simba ameweka wazi kuwa wamekuwa na kambi yenye mafanikio hivyo wanarejea kuendelea na maandalizi kwenye ardhi ya Tanzania.

“Timu ilikuwa kambini Misri na mafanikio yameonekana kwenye mechi za kirafiki pamoja na maandalizi kiujumla ambacho kimetokea huko ilikuwa ni furaha kwa kila mchezaji, benchi la ufundi.

“Wanarejea Tanzania kukamilisha maandalizi ya mwisho kuelekea kwenye tamasha la Simba Day tunaamini itakuwa ni siku nzuri kwelikweli hivyo mashabiki wawe tayari kwa ajili ya furaha na burudani zaidi.”