UCHAWI WA ALLY SALIM NA PENALTI UPO HAPA

MLINDA mlango wa Simba, Ally Salim, amefunguka kuwa siri kubwa ya kuokoa penalti tatu kati ya nne zilizopigwa na Yanga katika mchezo wa Fainali ya Ngao ya Jamii, ni maelekezo aliyopewa na kocha wao wa makipa, Daniel Cadena.

Salim jana Jumapili alifanikiwa kuibuka shujaa kwa kuokoa penalti tatu za Yanga zilizopigwa na Pacome Zouzoua, Yao Attohoula na Khalid Aucho na kuifanya Simba kuibuka na ushindi wa penalti 3-1.

Kipa huyo aliyeibuka shujaa dhidi ya Yanga, Salim amesema, “Kwanza namshukuru Mungu kwa ushindi huu muhimu kama timu, kwa kuwa pia ni mwanzo wa kutimiza malengo yetu ya msimu huu.

“Kuhusu siri ya mafanikio jambo kubwa ni kufuata kile ambacho benchi a ufundi na hususani kocha wetu wa makipa, Daniel Cadena alichonielekeza kwa kuwa kabla ya penalti mliona aliniita na kuniambia nini natakiwa kufanya.

“Kuhusu presha kwa kuwa wachezaji wenzangu walikosa, hapana, sikuwa na wasiwasi wowote, mara nyingi nimekuwa nikifanya mazoezi ya penalti, hivyo sikuwa na hofu, bali nilijua ninawajibika kufuta makosa ya wenzangu.”